Akili Mali

Sababu zilizomfanya aache mahindi, ahamie kilimo cha ‘managu’

Na JOHN NJOROGE August 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

ALIPOMTEMBELEA rafiki yake katika shamba la Matuiku, kilomita chache kutoka mji wa Elburgon mnamo 2020, Benson Muchai hakujua kwamba mazungumzo kati yao yangebadilisha kilimo chake cha mahindi alichokifanya kwa muda mrefu na kuanza kilimo cha mazao ya muda mfupi ambacho kingempa mauzo mazuri bila kutumia pesa nyingi mwishoni mwa msimu.

Muchai, 38, anasema mkulima huyo alikuwa akipanda mboga aina ya mnavu (managu) katika shamba lake la nusu ekari.

Rafikiye Muchai alimwambia kuwa kwa kila miezi mitatu hadi minne, alipokea takriban Sh1.5 milioni kutoka kwa mauzo, akiongeza kuwa kilimo hicho kilikuwa rahisi kwani hakina kazi nyingi na bei yake kwenye soko ilikuwa nzuri.

Alipomuuliza rafiki yake siri ya mafanikio hayo yalikuwa nini, alimjibu kuwa kwa kupata maji ya kutosha, mkulima yeyote anaweza kuwekeza na kustawi katika kilimo cha managu hata kwenye eneo dogo.

Baada ya kushauriana na mkewe, walikubaliana kubadilisha shamba lao la mahindi na kuanza kilimo cha managu kwenye nusu ekari ya shamba walilokodisha katika maeneo ya Elburgon, Kaunti ya Nakuru.

Wakati wa mahojiano hivi majuzi, Muchai alisema kuwa kwa mtaji wa Sh20,000, alikodisha shamba la nusu ekari kwa Sh7,500.

Alinunua gramu 100 za mbegu na mifuko mitano ya samadi ya mifugo ambayo aliisambaza shambani kabla ya kulima.

Alichanganya mbegu hizo na mfuko wa vumbi ya mbao na kupanda kwenye mitaro huku akizipa nafasi ya 15cm na baadaye kunyunyizia maji ya kutosha.

Mbegu hizo ziliota kati ya wiki mbili hadi tatu, kulingana na usambazaji wa maji. Katika wiki ya tatu, mkulima alinyunyizia shamba lake dawa za kumaliza magugu na kusambaza samadi zaidi shambani baada ya mwezi mmoja.

“Mboga za managu huwa tayari kuvunwa baada ya siku thelathini na wiki moja. Katika mavuno yangu ya kwanza, nilivuna kilo 800 na kuuza katika soko la ndani kwa Sh70 kwa kila kilo,” anasema Muchai, akiongeza kuwa mauzo aliyopata hayangelinganishwa na alichopata kila mwaka kutokana na mauzo ya gunia la mahindi la kilo 90 alilouza kwa Sh2,400 na Sh1,800 mtawalia kulingana na msimu.

Anaongeza kuwa wakati wa msimu mzuri, alikuwa akivuna kati ya magunia 25 na 30 ya mahindi kutoka kwa eneo hilo la nusu ekari kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita tofauti na kilimo cha managu ambapo wakulima wanaweza kuvuna zaidi ya kilo 1,500 kila wiki kwenye eneo sawia.

Muchai anasifia soko la mboga hizo ikilinganishwa na kilimo cha mahindi kwa sababu anauzia wateja moja kwa moja
Kilimo hicho kimemwezesha kununua shamba lake mwenyewe ambapo analima managu zaidi na mazao mengine, hulipa karo ya shule kwa watoto wake na kukidhi mahitaji mengine nyumbani.

Anaeleza kuwa kwa sasa huvuna zaidi ya kilo 2,500 wakati wa msimu mzuri au wa mvua huku kilo moja kwa sasa ikiuzwa kwa Sh50.

Baada ya kuvuna mboga kwa miezi minne mfululizo, Muchai hufanya mzunguko wa mazao kwa kupanda karoti, brokoli, maharagwe na viazi baadhi ya mazao mengine ya muda mfupi, lakini huhakikisha kuwa anaendelea kukuza managu katika eneo tofauti ili kuwadumisha wateja wake.

“Nimeongeza shamba langu la managu hadi ekari mbili na nusu kabla ya kufikia maono yangu ya kupanda hadi zaidi ya ekari tano katika miaka miwili ijayo mradi tu niwe na maji ya kutosha,” anasema.

Mboga hizo hutoa mbegu ambazo huvunwa na kuhifadhiwa kwa ajili ya kupanda kwa msimu ujao.

Anasema kuwa hii humfaidi kwa kuzalisha mbegu za kutosha bila kununua kutoka kwa maduka ya pembejeo. Tangu alipoanza kupanda managu kwa miaka sita iliyopita, Muchai anasema hajawahi kumbana na ugonjwa wowote unaoathiri mazao yake, mradi tu yanasimamiwa vizuri na kupewa virutubisho sahihi.

Kulingana na Sarah Kimani ambaye hupanda zao hilo kwenye robo ya shamba lake, anapata zaidi ya Sh 150,000 kutokana na mauzo kila mwezi, hasa wakati mvua inanyesha kwa wingi.

Aliongeza kuwa siku chache baada ya kutathmini hali ya shamba la Muchai, aliamua kuanza kilimo chake mwenyewe.

“Kwa miaka miwili iliyopita tangu nilipopanda managu, sijutii kwa sababu nimeweza kupata faida bila kutumia pesa nyingi shambani tofauti na mazao mengine kama vile mahindi na viazi ambapo nilikuwa nikitumia pesa nyingi. Mpango wangu ni kupanua shamba langu na kupanda zaidi ili kukidhi mahitaji ya wateja ambao wamezidi kuongezeka,” anaeleza Sarah.