Aladwa: ODM haitavuruga mkutano wa Linda Mwananchi Jacaranda
MBUNGE wa Makadara George Aladwa Ijumaa alisema ODM haina nia ya kuvuruga wala kuingilia mkutano wa Linda Mwananchi ambao utafanyika mnamo Jumapili katika uwanja wa Jacaranda, Nairobi.
Bw Aladwa alisema Linda Mwananchi ina haki ya kufanya shughuli zake za kisiasa na kuwafikishia wakazi wa Nairobi ujumbe wake.
Alisisitiza kuwa ushindani wa kisiasa unafaa kujikita katika sera na mawazo badala ya makabiliano kati ya wafuasi wa vyama.
“Linda Mwananchi iko huru kufanya mkutano wake na shughuli zake za kisiasa Nairobi. Kenya ni nchi ya kidemokrasia inayohakikisha kila kundi au mrengo wa kisiasa una haki ya kukusanyika, kuhamasisha wafuasi na kuwasilisha ajenda kwa wananchi,” akasema Bw Aladwa.
Aliongeza kuwa ODM Nairobi haina sababu ya kuingilia mkutano huo na haitafanya hivyo. Vinara wa Linda Mwananchi Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna, Gavana wa Siaya James Orengo na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino wanatarajiwa kuongoza mkutano huo wa Jacaranda.
“Waache wafanye mkutano wao na waambie wakazi wa Nairobi wanachosimamia na kile wanachonuia kuwapa Wakenya. Wananchi wana akili ya kusikiliza jumbe mbalimbali za kisiasa na kufanya maamuzi yao,” akasema Bw Aladwa.
Pia mbunge huyo alimpongeza Inspekta Jenerali wa Polisi Douglas Kanja kwa kujitolea kuhakikisha usalama unadumishwa wakati wa mkutano huo.
Alisema ODM Nairobi kwa sasa imejikita katika kuimarisha chama hicho jijini kupitia mikutano mbalimbali kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
“Lengo letu kama ODM Nairobi liko kwingine. Kwa sasa tunaendesha mpango wa kuimarisha chama katika maeneo yote ya Nairobi,” akasema mwenyekiti huyo wa ODM Nairobi.
Bw Aladwa alisema chama hicho pia kinajiandaa kwa sherehe za kuadhimisha mwaka moja baada ya kifo cha marehemu aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga.
Akizungumza kuhusu maandalizi ya uchaguzi wa 2027, Bw Aladwa aliwataka wafuasi wa ODM kuwa watulivu na kuepuka kuchokozwa na kuingia katika makabiliano yasiyo ya lazima.
“Hatuna chochote cha kuthibitisha kupitia vurugu au kuvuruga shughuli za wengine,” akasema.
Bw Aladwa pia alitoa wito kwa wafuasi wa Linda Mwananchi kuheshimu shughuli za ODM kama ambavyo chama chake kitaheshimu shughuli zao.
Alisema ODM itaendelea kuwafikia wananchi katika maeneobunge na wadi zote za Nairobi ili kueleza ajenda yake na kuimarisha chama kabla ya uchaguzi wa 2027.
“Nairobi ni yetu sote ni jiji kuu ambalo sauti na makundi mbalimbali ya kisiasa yanapaswa kuruhusiwa kufanya shughuli zao kwa uhuru na amani,” akasema.