Habari

Korti yazima mchakato wa zabuni ya karatasi za uchaguzi wa 2027

Na JOSEPH WANGUI September 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MZOZO wa kisheria umeibuka kuhusu kampuni zinazostahili kuchapisha karatasi za kura za uchaguzi wa 2027, huku Mahakama ikichunguza masharti ya zabuni ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).

Kampuni ya humu nchini, Oilmax Ventures Ltd, imewasilisha mzozo huo Mahakama Kuu baada ya Bodi ya Mapitio ya Ununuzi wa Umma (PPARB) kukataa malalamiko yake kuhusu masharti ya uzoefu na uwezo wa kifedha.

Mahakama imesimamisha mchakato wa zabuni hadi kesi hiyo itakapoamuliwa.

Mzozo huo unahusu zabuni iliyotangazwa na IEBC Agosti 11, 2026 ya kusambaza karatasi za kura, vifaa maalumu kwa wapigakura wenye ulemavu wa kuona, Sajili ya Wapigakura na fomu za kutangaza matokeo ya uchaguzi mkuu.

Zabuni hiyo ilihitaji kampuni zinazowania kuwa zimekamilisha angalau mikataba miwili ya awali ya uchapishaji wa stakabadhi za uchaguzi zenye alama za usalama, mmoja ukiwa wa angalau karatasi za kura milioni 150 ndani ya miaka mitano iliyopita.

Pia, zilitakiwa kuwa na wastani wa mapato ya Sh6 bilioni kwa mwaka 2023, 2024 na 2025, pamoja na uwezo wa kupata Sh10 bilioni kwa mtiririko wa kifedha wa kugharamia usambazaji.

Oilmax ilipinga masharti hayo ikisema ni ya kibaguzi, yenye kuondoa ushindani na yasiyolingana na zabuni hiyo.

PPARB ilikataa malalamiko hayo Septemba 3, ikisema Oilmax haikuthibitisha kuwa masharti hayo yalikuwa kinyume cha sheria.

Bodi hiyo ilikubali maelezo ya IEBC kwamba uchaguzi wa 2027 utahitaji takriban karatasi za kura milioni 168.

Ilibaini kuwa hitaji la karatasi milioni 150 lilikuwa sawa na asilimia 89.3 ya mahitaji hayo na lilihusiana na ukubwa wa zabuni.

Hata hivyo, Oilmax sasa imeibua suala jingine kuhusu sharti la asilimia 40 ya maudhui ya ndani katika zabuni hiyo.

Kampuni hiyo inasema kampuni za kimataifa zenye uwezo wa kuchapisha karatasi milioni 150 huenda zisitimize sharti la asilimia 40 ya ushiriki wa kampuni za Kenya.

Mkurugenzi wa Oilmax Mohammed Ali alisema angalau asilimia 40 ya mkataba ilipaswa kutekelezwa na watengenezaji wa Kenya au wakandarasi raia wa Kenya.

Kesi hiyo itatajwa Oktoba 7.