Wantam: ODM yamalizana na Sifuna licha ya nyota yake kung’aa
MZOZO wa miezi kadhaa kati ya ODM na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna umefikia kikomo baada ya Jopo la Kutatua Migogoro ya Vyama vya Kisiasa (PPDT) kutupilia mbali ombi lake la kutaka kubatilisha kuondolewa kwake kama Katibu Mkuu wa chama hicho.
Uamuzi huo wa Alhamisi wiki hii unafunga ukurasa muhimu katika safari ya kisiasa ya Bw Sifuna ndani ya ODM, chama ambacho alihudumu kama Katibu Mkuu kwa miaka minane tangu 2018.
Lakini zaidi ya nafasi ya Bw Sifuna, mzozo huo umeonyesha mpasuko mkubwa kuhusu mwelekeo wa ODM, nidhamu ya chama na nafasi ya viongozi wanaotofautiana na msimamo rasmi wa chama.
PPDT ilisema Kamati Kuu ya Kitaifa (NEC) ya ODM ilikuwa na mamlaka ya kuunda jopo maalum la kusikiliza tuhuma dhidi ya Bw Sifuna.
Jopo hilo pia lilibaini kuwa mwanasiasa huyo alipewa nafasi ya kujitetea kabla ya NEC kumwondoa katika wadhifa huo Juni 22, 2026.
Hii ilikuwa hatua ya pili katika mzozo huo.
Mnamo Juni 18, PPDT iliamua kuwa ODM ilikiuka haki ya Bw Sifuna ya kusikilizwa kwa haki ilipomwondoa kwa mara ya kwanza Februari 11, 2026.
Hata hivyo, chama kiliruhusiwa kuanza tena mchakato wa kinidhamu kwa kufuata katiba yake na sheria za vyama vya kisiasa.
ODM ilitumia nafasi hiyo kuendesha mchakato mwingine ambao sasa umeidhinishwa na PPDT.
Chanzo kikuu cha mzozo kilikuwa madai ya utovu wa nidhamu. Chama kilimtuhumu Bw Sifuna kwa kutoa matamshi yaliyopingana na misimamo rasmi ya ODM, kutohudhuria baadhi ya mikutano muhimu na kushiriki shughuli za kisiasa ambazo hazikuwa zimeidhinishwa na chama.
Miongoni mwa shughuli hizo ni mikutano ya Linda Mwananchi, vuguvugu ambalo limekuwa likimjenga katika siasa za upinzani.
Mvutano ulianza kuchukua sura mpya Julai 2025 baada ya Bw Sifuna kuonekana katika kipindi cha televisheni na kusema Makubaliano ya Ushirikiano kati ya ODM na UDA yalikuwa “yamekufa”.
Kauli hiyo haikupokelewa vyema na uongozi wa chama.
Aliyekuwa kiongozi wa ODM, Raila Odinga, wakati huo alisisitiza umuhimu wa Katibu Mkuu kufuata na kutetea misimamo rasmi ya chama anapozungumza hadharani.
Baada Raila kufariki, Sifuna aliendelea kushikilia msimamo wake na ODM ikamtumia notisi ya kujitetea. Seneta huyo alipinga notisi hiyo akisema haikuwa imeeleza kwa kina malalamishi dhidi yake.
Chama kilitoa maelezo zaidi na kuongeza muda wa mchakato wa kusikilizwa.
Wakili wa Bw Sifuna alifika mbele ya jopo la chama lakini akaibua pingamizi kuhusu uhalali na muundo wake kabla ya kujiondoa bila kujibu tuhuma zilizowasilishwa.
Jopo lilitupilia mbali pingamizi hizo na kupendekeza Bw Sifuna aondolewe. NEC baadaye ilikubali pendekezo hilo.
Katika kesi yake mpya, Bw Sifuna alisisitiza kuwa jopo hilo halikutambuliwa katika katiba ya ODM na hivyo halikuwa na mamlaka ya kushughulikia suala lake.
PPDT, hata hivyo, ilikubaliana na chama kwamba NEC inaweza kuunda kamati au majopo ya muda kushughulikia majukumu maalum kwa niaba yake.
Uamuzi huo sasa unaweka wazi kuwa kuondolewa kwa Bw Sifuna kama Katibu Mkuu wa ODM kumesalia.
Kwa ODM, huu ni ushindi kwa wale ambao hawakumtaka Sifuna kwa sababu ya kuwakosoa.
Kwa Bw Sifuna, hata hivyo, uamuzi huo unafungua swali la hatua yake inayofuata kisiasa.
Seneta huyo amekuwa mmoja wa wanasiasa wanaohusishwa na Linda Mwananchi, pamoja na Gavana wa Siaya James Orengo, Mbunge wa Embakasi East Babu Owino na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi.
Kwa hivyo, kuondoka kwake katika uongozi wa ODM kunatazamwa kama baraka kwa kuwa ushawishi wake umeongezeka kwa kasi.
Kwa upande mwingine, ODM sasa inakabiliwa na jukumu la kujenga upya uongozi wake na kueleza nafasi yake katika siasa za upinzani baada ya mzozo huo.
Kwa sasa, uamuzi wa PPDT umefunga mzozo wa Sifuna na ODM lakini haujazima nyota yake inayozidi kung’aa.