Uvumbuzi wa chakula maalum kufaa mifugo wakati wa kiangazi
HUKU kiangazi na ukame ukiendelea kuathiri wakulima hasa maeneo kame na nusu-kame (ASAL), teknolojia ya uongezaji malisho thamani kurefusha muda imegeuka kuwa tegemeo kwa wafugaji.
Wafugaji wanaokabiliwa na uhaba wa chakula cha mifugo wakati wa kiangazi sasa wanaweza kutumia lishe yenye virutubisho anuwai ya Sh300 pekee iliyovumbuliwa na kutengenezwa na Shirika la Utafiti wa Kilimo na Mifugo (KALRO) ili kusaidia mifugo.
Lishe hiyo iliyoundwa na tawi la KALRO, Muguga, Kiambu imesheheni molasi na urea. Molasi hutoa nishati, huku urea ikisambaza nitrojeni inayohitajika kwa mifugo.
Eric Too, mtafiti kutoka KALRO, anasema teknolojia hiyo inalenga kusaidia wafugaji hasa wakati wa ukame na kiangazi kirefu ambapo upatikanaji wa chakula cha mifugo huwa changamoto.
Too anasema chakula hicho maalum ni muhimu hasa katika maeneo yanayokabiliwa na ukame na uhaba wa malisho.

“Tumetengeneza bidhaa hii kusaidia wafugaji, hasa wakati wa kiangazi ambapo kuna changamoto ya upatikanaji wa chakula cha mifugo,” anasema.
Lishe hiyo yenye uzani wa kilo mbili, anahoji haina tofauti na chakula cha kawaida cha mifugo ikizingatiwa kuwa malighafi yaliyotumika ni yaleyale ya kawaida ila tu imeboreshwa.
Wafugaji wanashauriwa kuendelea kuwapa ng’ombe, mbuzi na kondoo chakula bora kama vile lucerne, Boma Rhodes na super Napier kabla ya kuwapa chakula hicho.
Lishe hiyo maalum ilikuwa kati ya teknolojia na chakula kilichovutia wafugaji wakati wa Maonyesho na Kongamano la Chakula cha Mifugo Afrika (AFEC) 2026 yaliyofanyika Nairobi kati Julai 15 na 16. Hafla hiyo iliandaliwa na Chama cha Watengenezaji na Wauzaji wa Chakula cha Mifugo Kenya (AKEFEMA), na kuleta pamoja kampuni na taasisi 200 kutoka nchi 27 ulimwenguni.
Too, kwenye mahojiano na ‘Akilimali’ alisema chakula hicho maalum husaidia mifugo kuboreshe mmeng’enyo.
“Ni bora zaidi kupewa mifugo saa za jioni, wakati mnyama amepumzika ili kusaidia mmeng’enyo na matumizi bora ya chakula alichokula wakati wa mchana,” akashauri.
Alidokeza kwamba utafiti umebaini kupungua kwa kiwango cha kinyesi baada ya mifugo kutumia lishe hiyo yenye virutubisho tele, hasa baada ya muda wa wiki moja hadi mbili. “Hali hii inaweza kuwa na manufaa kwa mazingira kwa sababu matumizi bora ya chakula yanaweza kusaidia kupunguza uzalishaji wa gesi ya methane,” Too anafafanua.

Eric Too kutoka Shirika la Utafiti na Maendeleo ya Kilimo Kenya (KALRO) akipanga chakula maalum cha mifugo kilichotengenezwa na shirika hilo la utafiti, wakati wa Mkutano wa Afrika wa Chakula cha Mifugo na Virutubisho vya Chakula cha Mifugo (AFEC) 2026 ulioandaliwa na Chama cha Watengenezaji wa Chakula cha Mifugo nchini Kenya (AKEFEMA) katika Hoteli ya Safari Park, Nairobi, Julai 15, 2026. PICHA|SAMMY WAWERU
Mifugo, hasa ng’ombe, wanahusishwa na uzalishaji wa gesi zinazochangia ongezeko la joto duniani. KALRO inaendelea kuboresha teknolojia hiyo kama mojawapo ya njia zinazoweza kusaidia wafugaji kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi huku wakiboresha lishe ya mifugo.
Hata hivyo, Too anasema utafiti zaidi na ukusanyaji wa data unahitajika kubaini kiwango kamili cha kupungua kwa gesi ya methane, kwani athari zinaweza kutofautiana kulingana na aina ya mnyama anayelishwa chakula hicho maalum.
Lishe hiyo imekuwa ikitafitiwa kwa zaidi ya miaka mitano na hutengenezwa katika tawi la KALRO, Muguga.
Kifungu kimoja cha chakula hicho chenye uzani wa kilo mbili kinauzwa Sh300, na kinaweza kutosha ng’ombe mmoja kwa muda wa takriban wiki mbili.