MAONI: Yaliyompata Kindiki yanaonesha uhuni wa kisiasa hauna mipaka
GHASIA ambazo zilishuhudiwa katika mkutano wa Naibu wa Rais Prof Kithure Kindiki katika Kaunti ya Embu zinaonyesha kuwa kiongozi yeyote awe serikalini au upinzani anaweza kuathiriwa na tabia hii mbovu ambapo mara nyingi vijana hutumiwa.
Kuna huu mtindo ambao umekuwa ukishuhudiwa ambapo baadhi ya wafuasi wa mirengo mbalimbali hufurahishwa uhuni unapokabili upande wasiounga kisiasa.
Wakati ambapo viongozi wa Linda Mwananchi walivamiwa Homa Bay mwezi uliopita, baadhi ya wafuasi wa Serikali Jumuishi walisherehekea na hata kuwarejelea baadhi ya viongozi ambao walitajwa kuhusika.
Kiongozi mmoja hata alirejelewa kama Ayatollah, jina la kiongozi wa kiimani wa Iran, linalotumiwa kuashiria utawala wa kiimla.
Hii ni kutokana na upangaji wa ghasia zilizozuka Homa Bay ambazo kiongozi huyo anahusishwa nazo.
Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen naye alizua kejeli kwa kushangaa kwa nini viongozi wa Linda Mwananchi walikuwa wakienda mahali ambapo walikuwa tayari wameambiwa kuna wahuni au megenge ya kisiasa.
Yaliyomkumba Prof Kindiki katika Kaunti ya Embu yanastahili kukemewa kwa kinywa kipana na walioratibu au kuwatumia vijana wanastahili kuchukuliwa hatua za kisheria.
Inasikitisha kuwa mtu mmoja aliaga dunia, wengine kujeruhiwa na hata magari kuteketezwa yakiwemo magari mawili ya wanahabari.
Kama mkutano wa mtu wa hadhi ya naibu rais unaweza kutibuliwa, sasa itakuwaje kwa mwaniaji wa kawaida ama kiongozi wa ngazi ya chini?
Hili jinamizi la uhuni halina mipaka na linaweza kuathiri kiongozi yeyote wala halifai kushabikiwa na upande mmoja linapokabili upande mwingine.
Jinsi viongozi wa Linda Mwananchi walivyohisi uchungu Homa Bay huku majeruhi na kifo kikiripotiwa ndivyo pia upande wa Prof Kindiki ulihisi uchungu na kuumia baada ya mkutano wao kuingiliwa.
Ingawa hivyo, tatizo katika suala hili lote ni wanasiasa na vijana na iwapo watajirekebisha na kuthamini demokrasia basi hivi visa vya ghasia havingekuwa vikiripotiwa.
Kupiga kura ni haki ya kila Mkenya na ni Mkenya huyo atakayeamua jinsi atakavyotekeleza wajibu huo iwe kiongozi ameandaa mkutano eneo lake au la.
Iwapo unahisi kwamba unaona humhitaji kiongozi, basi hakuna haja ya kuenda kwa mkutano wa mwanasiasa huyo na kuuvuruga.
Kufanya hivyo ndiko huzua makabiliano na maafisa wa usalama ambao vifo huishia kuripotiwa pamoja na majeraha.
Ndiyo, jinsi hali ilivyo vijana wengi hawana ajira ila kuhatarisha maisha kwa sababu ya mwanasiasa kisha ujeruhiwe au kuuawa si suluhu kwa tatizo hili ambalo limekuwepo miaka nenda miaka rudi.
Kinachoudhi ni kwamba viongozi huwapa vijana kati ya Sh500 na Sh2,000 ili kuenda kuzua ghasia kwenye mkutano wa kiongozi pinzani ilhali fedha hizo ni ndogo na hata haziwezi kuyabadilisha maisha yao.
Nguvu na haki ya kuwachagua viongozi iko katika kupiga kura wala si vurugu za kuzuia upande mmoja kuandaa mkutano wa kisiasa.
Mikutano ya Linda Mwananchi Nairobi na Rais William Ruto iliyofanyika jijini Kisumu kwa amani inastahili kutumiwa kama mfano kwa wanasiasa.
Viongozi wa Linda Mwananchi walihutubia mikutano mingi jijini na wakaenda zao naye Rais Ruto bado anaendelea na ziara yake Nyanza.
Ushindani wa kisiasa si uadui na kila mwanasiasa anastahili kuruhusiwa auze sera yake kisha wananchi waachwe waamue.