Maoni

MAONI: Rais Ruto alifanya vyema kufafanua binafsi suala la wageni nchini

Na BENSON MATHEKA September 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UFAFANUZI wa Rais William Ruto kwamba raia wa mataifa ya Afrika wako huru kuwekeza na kufanya kazi nchini Kenya kwa kuzingatia sheria inastahili.

Hii ilifuatia mjadala kuhusu wafanyabiashara wa kigeni nchini uliozua taharuki kubwa miongoni mwa wananchi na wageni wanaoishi hapa.

Wengine walifAsiri matamshi ya awali ya rais kuwa mwito wa kuwatenga au hata kuwafukuza wageni wanaojihusisha na biashara ndogo ndogo.

Fasiri hiyo ilisababisha hofu na hata visa vya vurugu katika baadhi ya maeneo.

Kwa kufafanua msimamo wake, Rais Ruto ameonyesha kwamba Kenya bado ni taifa linaloheshimu sheria, ushirikiano wa kikanda na misingi ya biashara huru.

Ukweli ni kwamba Kenya imefaidika kwa miaka mingi kutokana na uwekezaji kutoka mataifa jirani na sehemu nyingine za Afrika.

Wawekezaji hao wamechangia katika ukuaji wa uchumi, kuunda nafasi za ajira na kuimarisha mahusiano ya kibiashara katika ukanda huu.

Hata hivyo, ufafanuzi wa rais hauondoi haja ya serikali kushughulikia malalamishi halali ya wafanyabiashara wa humu nchini.

Wakenya wengi wamekuwa wakihisi kushinikizwa na ushindani kutoka kwa baadhi ya wageni wanaofanya biashara katika sekta ambazo kwa kawaida zimekuwa zikitegemewa na wananchi wa kipato cha chini.

Suluhisho la changamoto hiyo halipaswi kuwa chuki au mashambulizi dhidi ya wageni, bali kuwepo kwa sera wazi na utekelezaji wa sheria kwa haki kwa wote.

Ni muhimu kukumbuka kwamba Muungano wa Afrika, Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Comesa na Eneo Huru la Biashara la Afrika (AfCFTA) vinategemea ushirikiano na uhuru wa wananchi kufanya biashara na kuwekeza katika mataifa mbalimbali.

Kenya haiwezi kunufaika na masoko ya mataifa mengine huku ikifunga milango kwa raia wa nchi hizo.

Kwa hivyo, hatua ya Rais Ruto ya kusisitiza kuwa wageni wanaofuata sheria wanakaribishwa nchini ni ya busara.

Wakati huo huo, serikali inapaswa kuhakikisha sheria za biashara, uhamiaji na ajira zinatekelezwa sawasawa bila ubaguzi.

Kenya imejijengea jina kama taifa la ukarimu, biashara na uwekezaji. Sifa hizo zinapaswa kulindwa.

Ufafanuzi wa rais umesaidia kupunguza mvutano uliokuwa umeanza kujitokeza na kutoa mwelekeo unaohitajika katika mjadala huu muhimu wa kitaifa.