MAONI: Kenya yafaa iwe kielelezo cha undugu wa Afrika kwa vitendo
KENYA kwa mara nyingine imejipata katika hali ya kutatanisha na inayotishia hadhi na sifa yake Afrika na kwenye jukwaa la kimataifa, safari hii ikiwa ni zaidi ya siasa.
Ni mdahalo tata wa kufedhehesha kidiplomasia ambao kando na kuweka wananchi na taifa kwenye njiapanda, vilevile unawahatarisha Wakenya wanaoishi, kufanya kazi, au kusomea katika mataifa jirani hususan Afrika.
Kauli ya Rais Ruto kuhusu msako dhidi ya raia wa kigeni wanaoendesha biashara kwa njia haramu imesababisha visa vya kuhofisha ambapo Waafrika kutoka nchi jirani, wameshambuliwa, kujeruhiwa, biashara zao kuporwa au kuharibiwa.
Ukatili huu dhidi ya raia wa kigeni waliokimbilia nchini ama kuomba hifadhi au kusaka riziki unatekelezwa na wenyeji ambao wameishi nao pamoja kwa miaka mingi wengine hata wakioana na kujaaliwa watoto pamoja.
Kenya imekuwa mstari wa mbele barani na kimataifa kupigia debe umoja na udugu wa Waafrika, huku ikihimiza mataifa ya Afrika kuondoa vikwazo vya mipaka ili kuruhusu biashara na usafiri huru.
Hata katika matukio yasiyotuhusu moja kwa moja, Rais amejitokeza kutoa taarifa akilaani vikali nchi zinazoripotiwa kuendesha ubaguzi kama vile Urusi-Ukraine, Israeli-Palestine, na Iran.
Mwezi mmoja tu uliopita, Afrika Kusini ilikejeliwa mno na kutengwa kiasi cha Waafrika wenzao kuhiari kushangilia Canada badala ya timu yake ya kitaifa katika Kombe la Dunia 2026, baada ya kuwafurusha kikatili Waafrika.
Wakenya waliokuwa mstari wa mbele kudhihaki Afrika Kusini mitandaoni, sasa hawana pa kuweka nyuso zao wakitamani ardhi ipasuke iwameze mzimamzima huku masaibu sawia yakiwakabili.
Huenda amri ya rais ilidhamiriwa vyema kuhakikisha utekelezaji wa sheria zinazohusu uhamiaji, leseni na udhibiti wa biashara.
Kenya kama taifa huru ina kila haki na jukumu la kuhakikisha wafanyaiashara wote wanazingatia sheria.
Hata hivyo, agizo la rais, ama kwa bahati mbaya au kimaksudi, lilitafsiriwa visivyo na kuwatumbukiza Wakenya ghafla miongoni mwa mataifa yanayoendeleza ubaguzi kwa misingi ya asili.
Licha ya kubuni sera kuhusu masuala ya kigeni, kauli ya Rais Ruto, kwa mara nyingine, imeiweka Kenya kwenye mtanziko kidiplomasia, na kutishia nafasi yake kama kitovu cha kiuchumi na kidiplomasia.wageni
Utangamano barani utasalia ndoto iwapo mataifa wanachama wa EAC wataendelea kukosa kuaminiana.
Itakuwa unafiki kwa Kenya kuitisha ulinzi kwa Wakenya wanaoishi, kufanya kazi au kusomea nchi jirani au ulaya ilhali inawadhulumu Waafrika waliomo nchini.