Uhuru akubali uamuzi wa mahakama; aahidi kuachilia wadhifa wa Jubilee
RAIS mstaafu Uhuru Kenyatta ameondoa wasiwasi kuhusu mchakato wa kukabidhi uongozi wa chama cha Jubilee, akisema yuko tayari kufanya hivyo kwa uwazi, kwa mujibu wa sheria na katiba ya chama.
Kauli ya Uhuru ilijiri, siku chache baada ya Mahakama Kuu kusisitiza kwamba marais wastaafu hawapaswi kushikilia nyadhifa za uongozi wa vyama vya kisiasa kwa zaidi ya miezi sita baada ya kuondoka mamlakani.
Katika taarifa iliyotolewa Jumanne na Mkuu wa Mawasiliano wa ofisi yake Kanze Dena-Mararo, Bw Kenyatta alisema kuchelewa kwake kuachilia uenyekiti wa Jubilee kulitokana na mzozo wa ndani uliokuwa ukisubiri mwongozo wa kisheria.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, sasa hakuna kikwazo kinachozuia mchakato wa kubadilisha uongozi kufuatia ufafanuzi uliotolewa na mahakama.
“Rais mstaafu anathibitisha utayarifu wake kamili wa kuona mabadiliko ya uenyekiti yakikamilishwa kwa uwazi, kwa njia halali na kwa mujibu wa katiba ya chama. Anatazamia kuona taratibu za chama zikiendelea bila vikwazo,” ilisema taarifa hiyo.
Matamshi hayo yanajiri wakati Mahakama Kuu imesisitiza kuwa kifungu cha sheria kinachomzuia rais mstaafu kushikilia wadhifa wa uongozi katika chama cha kisiasa kwa zaidi ya miezi sita baada ya kuondoka afisini kinaendelea kutumika.
Jaji Lawrence Mugambi alitupilia mbali ombi lililokuwa likipinga Kifungu cha 6(1) cha Sheria ya Marupurupu ya Marais Wastaafu, akisema sheria hiyo haimzuii rais mstaafu kuwa mwanachama wa chama cha kisiasa au kushiriki shughuli za kisiasa.
Hata hivyo, mahakama ilisisitiza kuwa kinachokatazwa ni kuendelea kushikilia uongozi katika chama baada ya muda uliowekwa kisheria.
“Kinachozuiwa ni kushikilia nafasi ya uongozi katika chama kwa zaidi ya miezi sita baada ya kustaafu,” alisema Jaji Mugambi.
Uamuzi huo unaangazia upya mzozo wa uongozi wa Jubilee ulioanza baada ya Bw Kenyatta kuondoka mamlakani mwaka wa 2022 huku akiendelea kuwa kiongozi wa chama hicho.
Mwaka wa 2023, kundi moja ndani ya Jubilee lilitangaza nafasi yake kuwa wazi na kumteua Mbunge Maalum Sabina Chege kuwa kiongozi wa muda, likitaja sheria hiyo kama msingi wa hatua yake.
Hatua hiyo ilisababisha mvutano mkali kuhusu uongozi wa chama na mamlaka ya kufanya maamuzi muhimu.
Baadaye, Bw Kenyatta alirejea rasmi katika uongozi wa Jubilee mnamo Juni 2025 baada ya mahakama kubatilisha mabadiliko yaliyokuwa yamemweka Bi Chege pamoja na washirika wake madarakani.
Katika taarifa yake, Bw Kenyatta alisema anakaribisha sura mpya ya Jubilee na kizazi kipya cha viongozi watakaochukua usukani wa chama.
“Uhuru Kenyatta anakaribisha sura mpya ya Jubilee iliyojengwa juu ya utawala wa sheria, ikiongozwa na katiba ya chama na kuendelezwa na kizazi kijacho cha viongozi,” ilisema taarifa hiyo.