Siasa

Omar: Sikusema tutatumia wafu kutupigia kura, nilisema watu waamke wajitokeze kupiga kura

Na NDUBI MOTURI, BENSON MATHEKA September 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KATIBU Mkuu wa Chama cha UDA, Hassan Omar, amejitetea dhidi ya madai kwamba aliwahimiza wafu kumpigia kura Rais William Ruto katika uchaguzi mkuu ujao, akisema kauli zake zilitafsiriwa vibaya na kutolewa nje ya muktadha wake kisiasa.

Akizungumza kuhusu mjadala uliotokea baada ya matamshi yake ya hivi majuzi, Bw Omar alisema wanasiasa hasa wa kutoka pwani, mara nyingi hutumia methali, tamathali za semi na kejeli kuwasilisha ujumbe wao kwa wananchi, na kwamba watu wasiofahamu mtindo wa mawasiliano wa Pwani walikosea kuelewa alichomaanisha.

“Tunatumia tamathali za semi, methali na kejeli katika siasa. Ninavyozungumza Nairobi si jinsi ninavyozungumza Mombasa ninakotoka. Watu wasioelewa jinsi tunavyozungumza Mombasa wanapaswa kunyamaza,” alisema.

Kiongozi huyo wa UDA alisisitiza kuwa chama chake hakitegemei kura zisizo halali bali kinaamini kitapata ushindi kupitia kura za wananchi wanaojitokeza kupiga kura.

“Nina uhakika zaidi ya shaka yoyote kwamba William Ruto atachaguliwa tena. Tunataka kujenga ushindi ambao hauwezi kutikiswa. Hatuhitaji kura za wafu. Tutapigiwa kura na watu walio hai,” alisema.

Bw Omar alieleza kuwa matamshi yake yalilenga kuhamasisha wananchi, hasa katika Kaunti ya Mombasa, kujitokeza kwa wingi wakati wa uchaguzi.

Alibainisha kwamba uchaguzi mkuu wa mwaka 2022 ulikuwa na idadi ndogo ya wapigakura katika eneo hilo, hali ambayo alisema inahitaji kubadilika ikiwa Rais Ruto atapata ushindi mkubwa.

“Mombasa ilikuwa na asilimia 40 pekee ya wapigakura waliojitokeza mwaka 2022. Nilichomaanisha ni kwamba watu wanapaswa kuamka na kujitokeza kuhakikisha tunapatia William Ruto ushindi,” alisema.

Kwa mujibu wa Bw Omar, kuunga mkono rais kwa maneno pekee hakutoshi bila wananchi kujiandikisha na kushiriki kikamilifu katika uchaguzi.

“Kumpenda rais ni jambo moja, lakini kujisajili na kumpigia kura ni jambo jingine. Nilinukuliwa nje ya muktadha,” aliongeza.

Aidha, alilaumu baadhi ya watumiaji wa mitandao ya kijamii kwa kupotosha kauli zake kwa maslahi ya kisiasa.

“Inasikitisha sana kuona yanayoendelea kwenye mitandao ya kijamii. Wapo waliochukua fursa ya kupotosha maneno yangu ili kutimiza malengo yao ya kisiasa,” alisema.

Katibu Mkuu huyo alisema UDA haina hofu ya kushindwa katika uchaguzi ujao, bali ina wasiwasi kuwa wapinzani wanaweza kuibua madai na visingizio mbalimbali wakishindwa.

“Sisi hatuogopi kushindwa uchaguzini. Tunachohofia ni kwamba tukishinda, wale watakaoshindwa wataanza kuja na kila aina ya visingizio,” alisema.

Kauli za Bw Omar zinajiri wakati shughuli za kisiasa zinaanza kushika kasi kuelekea uchaguzi mkuu ujao, huku vyama vikiongeza juhudi za kuhamasisha wapigakura na kuimarisha misingi yao katika maeneo mbalimbali nchini.