Takwimu za CBK zaonyesha Wakenya wanakopa sana kumudu mahitaji ya kila siku
HALI ngumu ya maisha imesukuma mamilioni ya Wakenya kutafuta mikopo ya kidijitali ili kukidhi mahitaji ya kila siku, huku zaidi ya akaunti milioni nane zikikopa zaidi ya Sh150 bilioni.
Takwimu za Benki Kuu ya Kenya (CBK) zinaonyesha kuwa mikopo hiyo mingi haitumiki kuanzisha biashara au kuwekeza, bali kugharamia matumizi na mahitaji ya kimsingi ya maisha.
Mkurugenzi Mkuu wa Metropol Credit Reference Bureau, Gideon Kipyakwai, alisema Wakenya wanakopa kwa viwango vya juu kutokana na ukosefu wa imani unaowazuia wengi kupata mikopo kutoka taasisi rasmi za kifedha.
Alisema hali hiyo imewasukuma wengi kugeukia wakopeshaji wa kidijitali baada ya kufungiwa nje ya mifumo ya kawaida ya benki na taasisi nyingine za mikopo.
“Taasisi za mikopo ya kidijitali zimeziba pengo la upatikanaji wa mikopo lililoachwa na mifumo ya jadi, huku Wakenya wakikopa mabilioni kwa kubofya kitufe kwenye simu zao,” alisema Kipyakwai.
Akizungumza pembezoni mwa Kongamano la Tatu la Kitaifa la Soko la Mikopo lililofanyika Naivasha, Kipyakwai alisema CBK imeidhinisha taasisi 300 za ukopeshaji, huku mamia ya zingine zikisubiri idhini.
Alizitaka taasisi hizo kutumia data na teknolojia za kisasa kutathmini uwezo wa wakopaji, badala ya kutegemea mbinu zinazoweza kuongeza viwango vya kushindwa kulipa mikopo.
Kipyakwai alisema zaidi ya asilimia 80 ya Wakenya watu wazima wamesajiliwa katika Credit Reference Bureau, inayotumiwa kutathmini uwezo wa mtu kukopa na kulipa.
Alisema ushirikishaji wa kifedha nchini umefikia asilimia 84, huku mikopo kwa biashara ndogo na za kati ikiwa asilimia 30.
Hata hivyo, aliyekuwa Katibu wa Wizara ya ICT, Dkt Bitange Ndemo, alisema ukweli kwamba Wakenya wengi wanakopa kwa matumizi badala ya uwekezaji ni ishara ya hali ngumu ya uchumi.
Ndemo alitaka udhibiti uimarishwe ili kukabiliana na wakopeshaji haramu wanaotumia mbinu zisizo za kimaadili na kuwanyanyasa wateja.
Alisisitiza pia umuhimu wa matumizi ya Akili Unde (AI) na data kubwa katika kutathmini uwezo wa wakopaji, huku akionya kuwa ulinzi wa data ni muhimu katika ukuaji wa sekta hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa Financial Sector Deepening Kenya (FSD Kenya), Rashmi Pillai, alisema sekta hiyo inahitaji huduma zinazoaminika zaidi na zinazokidhi mahitaji ya wateja.
Kwa mujibu wa kanuni zilizopitishwa, wakopeshaji wote wenye leseni wanapaswa kuzingatia sheria za ulinzi wa data, kutoa maelezo kamili kuhusu gharama za mikopo na kutumia mbinu za haki katika kukusanya madeni.