MAONI: Linda Mwananchi isitanue misuli ya maslahi, ijali wapendavyo raia
MKUTANO wa Linda Mwananchi ulioandaliwa katika uwanja wa Jacaranda, Nairobi ni kati ya mikutano mikubwa ambayo imetia wasiwasi serikali ya Rais William Ruto na Muungano wa upinzani unaojumuisha Kalonzo Musyoka, Rigathi Gachagua, Eugene Wamalwa, Dkt Fred Matiangi, Justin Muturi na Bi Martha Karua.
Kundi la Seneta wa Nairobi Edwin Watenya Sifuna liliteka Nairobi kwa kishindo kikubwa.
Magazeti yakapata masoko, redio zikawataja vinara bila ukomo na vijana wa mitandao ya kijamii wakachapisha matukio muhimu ya maeneo walikofika wanasiasa hao wakijumuisha Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, Gavana wa Siaya James Orengo, mwenzake wa Trans Nzoia George Natembeya kati ya wengine.
Hata hivyo, katika chereko zote hizo, kuna vita vya chini kwa chini kuhusu ni nani anayestahili kuwa kiongozi wa Linda Mwananchi na pia mgombea Urais.
Tofauti hizi kati ya Sifuna, Babu Owino na James Orengo huenda zikaliwacha vuguvugu hilo na majeraha makubwa kwa sababu jeshi kubwa la vijana lilikuwa nyuma yake.
Nyufa katika ukuta huo pia zitagawanya hamu ya vijana kwa mapande tofauti na kumpa Rais Ruto nafasi rahisi kutwaa Urais kwa mara nyingine.
Vivyo hivyo, kukiwa na mgawanyiko hapo katika Linda Mwananchi muungano wa United Opposition utaanza kujigamba kuwa huo ndio uliokuwa upinzani halisi wa kukabiliana na Rais Ruto.
Ikumbukwe kuwa kundi hilo la vijana lina msukumo kiasi kwamba mabalozi wa nchi tofauti wanakutana na Sifuna kwa misingi kuwa athari zake zimekuwa kubwa katika jicho la diplomasia na uwezekano wa yeye kuwa Rais wa sita wa Jamhuri ya Kenya upo.
Hoja nyingine inayojitokeza katika vurugumechi hii kati ya Sifuna, Orengo na Babu Owino ni kuwa walijitenga na chama cha ODM kwa kile walichodai kuwa ukosefu wa demokrasia.
Je, vitendo vyao kwa sasa vinaakisi uzingativu wa demokrasia ama ni misuli ya masilahi?
Waliosalia katika chama cha ODM kama mwenyekiti wake Gladys Wanga na kiongozi wa chama Oburu Oginga kwa sasa wanapiga sherehe kutokana na msukosuko huu ndani ya Linda Mwananchi.
Kabla uchaguzi mkuu wa 2002, mizozo kama hii ilikuwa katika muungano wa NAK kwanza kati ya Mwai Kibaki, Wamalwa Kijana na Charity Ngilu.
Kila mmoja alikuwa anataka kuwa Rais lakini wadau wakakubalia kuwa Kibaki apeperushe bendera, Wamalwa awe naibu wake.
Hii iliwafanya kuaminika na hata Raila Odinga akajiunga nao bila masharti. Kundi la Sifuna litashawishi muungano wa upinzani kuliunga mkono tu endapo litakuwa na msimamo, vinginevyo safari ya kumpeleka Ruto Sugoi hatakuwa rahisi.
Paul Nabiswa ni mhariri, NTV