Mashabiki wakerwa na kipigo cha Man United
MASHABIKI wenye huzuni wa Manchester United walishuhudia jambo ambalo halijawahi kutokea katika uwanja wa Old Trafford kwa nusu karne Jumatano.
Hii ni baada ya timu yao kupoteza 3-2 nyumbani dhidi ya Brighton & Hove Albion katika raundi ya tatu ya Carabao, licha ya kuongoza kwa mabao mawili.
Mara ya mwisho United kupoteza nyumbani baada ya kuongoza kwa mabao mawili ilikuwa Septemba 1976, Tottenham Hotspur iliposhinda kwa matokeo kama hayo ya 3-2.
Brighton ilifuzu kwa raundi ya 16 bora, huku kichapo hicho kikiwa pigo jingine kwa United, ambao walipoteza kwa 1-0 dhidi ya wapinzani wao Manchester City katika mechi yenye utata ya Ligi Kuu Uingereza (EPL) wikendi iliyopita.
United kwa sasa iko katika nafasi ya 13 ikiwa na ushindi mmoja katika mechi nne.
United ilifunga mabao mawili katika dakika nne za kipindi cha pili baada ya kijana Shea Lacey kuwapa uongozi dakika ya nane, kabla ya Mason Mount kuongeza bao la pili dakika mbili baadaye.
Charalampos Kostoulas aliifungia Brighton bao la kwanza katika muda wa nyongeza wa kipindi cha kwanza, kabla ya Pascal Gross kusawazisha dakika ya 65 na Maxim De Cuyper kufunga bao la ushindi dakika ya 69.
Mashabiki wa United waliwazomea wachezaji wao baada ya kipenga cha mwisho.
“Hatuwezi kukubali matokeo kama haya na mimi ndio najukumika na nafaa kuwajibishwa kwa hili. Mchezo wetu kuelekea mwisho wa kipindi cha pili ulikuwa duni mno,” Kocha Michael Carrick akasema baada ya mchuano huo.
Hiki kilikuwa kichapo cha tatu mfululizo cha United katika mashindano yote msimu huu. Msimu uliopita, waliondolewa katika raundi ya pili ya Carabao kupitia mikwaju ya penalti na Grimsby Town, ambayo inashiriki ligi ya daraja la nne,
Pia walipoteza 2-1 nyumbani dhidi ya Brighton katika raundi ya tatu ya FA Cup Januari.
Msimu uliopita ulikuwa wa kwanza tangu 1981-82 ambapo United ilishindwa kufika raundi yoyote katika FA na Carabao.