Habari za Kitaifa

Mikutano ya kisiasa yaendelea kuandamana na majonzi, 11 wakiangamia

September 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TAKRIBAN watu 11 wamepoteza maisha katika ghasia na matukio mengine yanayohusishwa na mikutano ya kisiasa nchini tangu Februari, huku mikutano iliyokusudiwa kurai wapigakura ikigeuka kuwa hatari Kenya inapokaribia Uchaguzi Mkuu wa Agosti 10, 2027.

Vifo hivyo vimetokea Nairobi, Homa Bay, Kisumu, Kisii, Vihiga, Kajiado na Embu, ambapo waathiriwa waliuawa au kujeruhiwa vibaya katika visa vya kupigwa risasi, kudungwa visu, kushambuliwa na makundi ya watu na mapigano kati ya polisi na raia.

Mikutano ya kisiasa imezidi kuandamana na mapigano, uharibifu wa mali na madai ya kuwepo kwa vijana wanaotumiwa kufanya vurugu.

Katika Kaunti ya Nairobi, miili mitatu ambayo haikuwa imetambuliwa awali ilipelekwa Nairobi Funeral Home na polisi baada ya mkutano wa Linda Mwananchi wa Jumapili iliyopita ulioanzia katikati ya jiji na kumalizikia Jacaranda Grounds.

Familia za waathiriwa zimekanusha madai yaliyoenezwa mitandaoni kwamba waliuawa baada ya kukamatwa wakiiba simu katika Barabara ya Jogoo.

“Kaka yangu, Joseph Omondi Shikuku, hajawahi kumwibia mtu yeyote. Yeye ni mtu mwema aliyekuwa akiendesha biashara ya kuuza nguo za mitumba Umoja 2. Kila kinachosemwa kwenye mitandao ya kijamii si kweli kabisa na sisi kama familia tumeumia,” alisema dadake, Mercy Awino Shikhukhu.

Uchunguzi wa baada ya kifo ulionyesha kuwa Omondi alifariki kutokana na majeraha kwenye fuvu la kichwa.

Familia inashuku huenda alisukumwa kutoka kwenye daraja la waenda kwa miguu na watu ambao hawakutambuliwa.

Brandon Ong’or, 19, pia alifariki Jumapili. Mama yake, Hellen Ong’or, alisema mwanawe hakuwahi kuiba bali alituhumiwa kuwa mwizi na mfuasi wa kundi pinzani la kisiasa.

Mkuu wa Polisi wa Buruburu, Boniface Lomuk, alithibitisha kupatikana kwa miili hiyo na kusema waathiriwa walidaiwa kushambuliwa na wakazi waliowalaumu kwa kuiba simu za waliohudhuria mkutano.

Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, alilaani ghasia hizo na kusema siasa hazipaswi kuwa sababu ya watu kupoteza maisha.

Vifo hivyo vilitokea siku chache baada ya watu wawili, Mike Macharia, 23, na Moses Munene, 30, kupigwa risasi wakati wa mapigano katika mkutano uliohutubiwa na Naibu Rais Kithure Kindiki katika Uwanja wa Nembure, Embu.

Vijana waliokuwa nje ya uwanja walirusha mawe huku polisi wa kukabiliana na ghasia wakiwatawanya. Mapigano hayo yalidumu kwa saa kadhaa na magari sita yakachomwa moto.

Kaunti ya Homa Bay pia ilirekodi vifo viwili Agosti 16 wakati wa ghasia zilizohusishwa na mkutano wa Linda Mwananchi.

Konstebo Jim Richardson Onkundi, 36, alipigwa kichwani kwa jiwe, na gari lake likagonga jengo. Norine Nalangwa aligongwa na gari lililokuwa likienda kwa kasi alipokuwa akivuka barabara.

Na Kaunti ya Kisumu, Dickson Oduor alifariki Julai 12 baada ya kudungwa visu wakati wa makabiliano kati ya wafuasi wa Linda Mwananchi na wanaounga mkono serikali.

Katika kaunti ya Kisii, Vincent Osiemo, maarufu Mapinduzi, alifariki Julai 3 baada ya kuanguka kutoka kwa gari lililokuwa likitoroka mawe wakati wa mapigano.

Katika kisa kingine huko Vihiga, mwendesha boda boda George Otobe aliuawa na kundi la watu Februari 21, huku Vincent Ayomo akipigwa risasi na kufariki Kitengela mwezi huo huo.

Ghasia hizo zimeibua wasiwasi kuhusu usalama kuelekea uchaguzi wa 2027.

Rais William Ruto, mwezi uliopita alikosoa washukiwa wa vurugu za kisiasa wanavyoshughulikiwa, akisema baadhi hupewa dhamana ndogo na kurejea kwenye mikutano.

IEBC imesema itachukua hatua dhidi ya wanaokiuka sheria za uchaguzi.

Mwenyekiti wake Erastus Ethekon, amesema tume hiyo, haina mamlaka ya kutekeleza usalama na inategemea idara za usalama.

Kipindi rasmi cha kampeni kitaanza Mei 29, 2027 na kumalizika Agosti 7.

Hata hivyo, miezi kadhaa kabla ya kampeni kuanza rasmi, mikutano ya kisiasa tayari imehusishwa na vifo.