• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 5:46 PM
Uchomaji makaa wapigwa marufuku Narok

Uchomaji makaa wapigwa marufuku Narok

Na GEORGE SAYAGIE

SERIKALI ya kaunti ya Narok, imepiga marufuku uchomaji wa makaa kwa muda usiojulikana kufuatia ukataji miti katika misitu ambao umesababisha Kenya kuathiriwa na mabadiliko ya hali ya hewa.

Kaunti za Kitui na Machakos pia zimepiga marufuku uchomaji wa makaa.

Hatua hii inajiri siku mbili baada ya Naibu Rais William Ruto kusimamisha ukataji miti katika misitu yote nchini kwa miezi mitatu ijayo.
Gavana Samuel Tunai aliagiza uchomaji wa makaa kusitishwa mara moja.

Aidha, alipiga marufuku usafirishaji wa makaa katika kaunti hiyo na kuagiza maafisa wa usalama kuhakikisha marufuku hiyo imetekelezwa.

Akiandamana na kamishna mpya wa kaunti hiyo Bw George Natembea na kamanda wa polisi Thomas Ngeiywa, Bw Tunai aliwataka polisi kusaka wanaofanya biashara ya makaa.

Alitangaza marufuku hiyo baada ya kukutana na makamanda wa polisi, wakuu wa wilaya, maafisa wa misitu, maafisa wa shirika la kulinda wanyama pori na maafisa wa ujasusi pamoja wale wa upelelezi wa jinai katika hoteli ya Lexington mnamo Jumapili.

Kwenye taarifa kwa wanahabari, Bw Tunai aliagiza ukataji miti katika misitu ya Mau, Nyakweri eneo la Transmara, Enoosupukia ulioko Narok Mashariki na Loita ulioko Narok Kusini isitishwe mara moja akisema ni haramu.

 

Kufurushwa

“Kutakuwa na msako mkali kuhakikisha wakataji miti katika maeneo haya wamefurushwa na watakaokiuka sheria watakabiliwa vikali,” alisema Bw Tunai.

Aliwaagiza wakazi kuripoti vitendo vya ukataji miti na uchomaji makaa kwa polisi. Alipiga marufuku usafirishaji wa makaa mchana na usiku kwa magari au njia yoyote ile.

Kaunti hiyo inaongoza kwa utoaji wa makaa ikifuatwa na Kajiado.

Watetezi wa mazingira wamekuwa wakionya kwamba misitu asili kama Mau, Nywakweri, Loita, Aitong na Naimina-Enkiyo, ambayo ni chanzo cha mito mingi inaangamia kufuatia shughuli za binadamu. Ukataji miti katika misitu hiyo umesababisha kiwango cha maji katika mito inayoanzia misitu hiyo kupungua.

Kulingana na takwimu za shirika la kulinda misitu nchini kaunti ya Narok ina ekari 139, 298 za misitu ikiwa ni asilimia 16.6 ya misitu yote nchini. Ekari 52,239 zinasimamiwa na KFS na 87,050 zinasimamiwa na serikali ya kaunti hiyo.

Kaunti ya Narok inatoa tani 25 milioni za makaa kila mwaka na uchomaji makaa hayo unasemekana kuwa chanzo cha kuharibiwa kwa msitu wa Mau.

 

You can share this post!

Wasiwasi wanawake wengi kujihusisha na ugaidi

Wakenya kuhesabiwa idadi Agosti 2019

adminleo