• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 6:50 AM
Madaktari 2,275 wafutwa kwenye sajili ya KMPDB

Madaktari 2,275 wafutwa kwenye sajili ya KMPDB

Na PETER MBURU

BODI ya Kusimamia Madaktari Nchini (KMPDB) Jumatano iliwaondoa madaktari 2,275 kutoka kwa sajili yake baada yao kukosa kuchukua leseni za kuhudumu mwaka huu.

Madaktari hao, wakiwa ni pamoja na 212 wa meno na 2,063 wa aina zingine kutoka hospitali za umma na za kibinafsi sasa hawatahudumu tena, hadi warejeshwe katika sajili hiyo, ambayo kila daktari anayefanya kazi humu nchini sharti awe ameorodheshwa hapo.

Kupitia tangazo lililochapishwa katika magazeti jana, Afisa Mkuu Mtendaji wa KMPDB, Daniel Yumbya alisema, madaktari wanaotaka kurejeshwa katika sajili hiyo sasa watatuma maombi kupata vyeti vya kuhudumu mwaka huu.

Bw Yumbya alisema kuwa bodi hiyo ilikutana mnamo Machi 29 na ikaamua kuwaondoa madaktari hao kutoka kwa sajili yake, kwa kuwa walikosa kutuma maombi wapewe vyeti vya mwaka huu vya kuendelea kuhudumu.

Kulingana na sehemu ya 14 ya sheria kuhusu uhudumu wa madaktari nchini “hakuna daktari anaruhusiwa kufanya kazi katika hospitali ya kibinafsi bila leseni kutoka kwa bodi ya madaktari.”

Sheria hiyo aidha inasema kuwa muda wa leseni hiyo kufanya kazi utakuwa ukiamuliwa na Mkurugenzi wa Matibabu nchini kwa ushirikiano na bodi hiyo.

Katika orodha ya madaktari, waliong’olewa kutoka sajili hiyo, baadhi yao hawajawahi kupokea leseni kutoka kwa bodi hiyo tangu 2015, japo wengi wao walipokea mwaka uliopita.

Madaktari kutoka maeneo tofauti ya nchi, yakihusisha Nairobi, Eldoret, Kisumu, Mombasa, Nandi, Bomet na mengine mengi waliathirika.

Hatua hiyo ya bodi ya madaktari aidha imetokea baada ya kufanya ukaguzi katika vituo vya afya nchini kwa miezi kadhaa na pia kuamrishwa kufungwa kwa vituo ambavyo havikuwa vimehitimu kutoa huduma za afya.

Bw Yumbya awali mwaka huu alieleza Taifa Leo kuwa, KMPDB ilikuwa ikishirikiana na asasi zingine kama ile ya wauguzi na maafisa wa kliniki kuendesha oparesheni za kuwasaka watu wanaoendesha kliniki kinyume na sheria.

“Mwaka huu pekee, tunalenga kukagua zaidi ya vituo 1,000 vya afya kwa ushirikiano na mamlaka zingine ili kubaini vifaa vilivyopo na huduma zinazotolewa. Kila kituo ambacho hakina leseni tunafunga,” akasema Bw Yumbya.

Hatua hiyo ya KMPDB inafuatia miezi minne tu baada ya serikali kuzindua Mradi wa Huduma ya Matibabu ya Bei Nafuu kwa Wote (UHC) unaoendelea kufanyiwa majaribio katika kaunti nne; Machakos, Nyeri, Isiolo na Kisumu.

Bila leseni, daktari haruhusiwi kutoa huduma za matibabu hivyo hatua hiyo ya KMPDB huenda ikatatiza mradi huo wa UHC.Kwa sasa, Kenya ina uhaba wa madaktari na wataalamu wa kutibu meno, kila daktari anatibu wagonjwa 16,000.

Shirika la Afya Duniani (WHO) linapendekeza angalau madaktari watatu watibu 20,000. Kuna madaktari 7,433 waliosajiliwa nchini Kenya ambao wanatibu zaidi ya Wakenya 40 milioni.

You can share this post!

Aliyemtishia ripota wa NMG azuiliwa na polisi

Bastola zaibwa polisi wakishabikia mechi

adminleo