• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 9:50 AM
‘Kieleweke’ wamuumbua Ruto kuhusu ufisadi

‘Kieleweke’ wamuumbua Ruto kuhusu ufisadi

Na CECIL ODONGO

MAOMBI yaliyoandaliwa na Muungano wa Vyama vya Wafanyakazi (COTU), Jumapili yaligeuka kuwa jukwaa la wanasiasa wa kundi la Kieleweke kuwavamia wenzao wa Tangatanga ambao wanamvumisha Naibu Rais Willam Ruto.

Wabunge waliohutubu wakati wa maombi hayo yaliyoandaliwa kwenye Kanisa la ACK la St Stephen Cathderal, walimwomba Rais Uhuru Kenyatta kuzidisha vita dhidi ya ufisadi huku wakisifu hatua ya wiki jana ya Kanisa la Kianglikana kusitisha michango ya Harambee.

Mbunge Maalum Maina Kamanda alianzisha mjadala huo kwa kusema viongozi wafisadi nchini wanajulikana peupe na wakati umewadia kwa asasi za kisheria kuwajibika na kuwakamata wahusika.

“Nasifu hatua ya kiongozi wa ACK kukomesha Harambee kwa sababu wanasiasa wanaoleta mabilioni kanisani tunajua ni wafisadi wala hawajapata pesa hizo kwa njia ya ukweli. Hapa Kenya hata ukimuuliza mtoto mdogo kiongozi fisadi zaidi, atakuambia au akuandikie jina la kiongozi fulani pekee,” akasema Bw Kamanda.

Katibu wa COTU Francis Atwoli naye kwa mara nyingine alianika tofauti kati yake na Dkt Ruto, akidai hawezi kushinda kiti cha urais mwaka wa 2022 kwa sababu hawezi kupita mtihani wa maadili.

“Kama hamjatubu, kama hamjakomesha ubabe wenu kwa kutumia kifua, mwaniaji mnayeunga mkono kwa jina la William Ruto hatakuwa Rais mwaka 2022. Ningependa kushukuru serikali ya Rais Uhuru Kenyatta kwa kutoa ulinzi kwetu baada ya baadhi ya wanasiasa maarufu kupanga kuvuruga mkutano wa Lebadei kesho. Mimi nilianza kuhesabu pesa ya mshahara zamani, tafadhali usituambie wewe ni tajiri,” akasema Bw Atwoli.

“Ile serikali ya 2022, watakuwemo Kalonzo Musyoka, Gideon Moi, Musalia Mudavadi, Hassan Joho mimi sitakuwa kwenye serikali kwa sababu siwanii cheo cha kisiasa hata watu wa mkoa wa Kati watakuwa ndani,” akaongeza Atwoli kwenye matamashi makali dhidi ya Dkt Ruto.

Mbunge wa Igembe Kaskazini Maoka Maore pia aliwashutumu wanasiasa wanaotatiza Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) na Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) zinapotekeleza kazi zao.

Hata hivyo, hisia kali zilitanda kanisani humo, pale tofauti za wazi zilipodhihirika kati ya Gavana wa Nairobi Mike Sonko na Mabw Kamanda na Peter Kenneth kuhusu uongozi wa jiji. Bw Sonko aliyeonekana kuhamaki aliwahusisha wawili hao na baadhi ya sakata za ufisadi miaka ya nyuma na hata kuwaonya dhidi ya kumdharau na kukosoa serikali yake bila sababu.

Kinara wa Chama cha Wiper Kalonzo Musyoka akigusia visa dhidi ya ufisadi alisema uovu huo unaporomosha uchumi wa nchi.

You can share this post!

Walioasi Al Shabaab sasa wajiunga na magenge Pwani

Shule zafunguliwa mtaala mpya ukitekelezwa

adminleo