• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
ONYANGO: Idadi kubwa ya vijana waliopo magerezani inashtua sana

ONYANGO: Idadi kubwa ya vijana waliopo magerezani inashtua sana

Na LEONARD ONYANGO

RIPOTI kuhusu Hali ya Uchumi ya 2019 iliyotolewa na Shirika la Takwimu nchini (KNBS) wiki iliyopita , inafaa kushtua serikali pamoja na wazazi.

Ripoti hiyo ilipotolewa, vyombo vya habari viliangazia tatizo la ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana licha ya uchumi kuonekana ‘kukua’.

Kulingana na ripoti hiyo, serikali ya Jubilee imefanikiwa kubuni nafasi milioni 1.8 za kazi pekee tangu ilipochukua hatamu za uongozi mnamo 2013, huku mamilioni ya watu wakiwa hawana kazi.

Lakini suala ambalo halikupewa uzito na wanahabari ni kuhusu idadi kubwa ya vijana wa chini ya umri wa miaka 25 wanaotumikia vifungo magerezani.

Ripoti hiyo ya KNBS inaonyesha kuwa karibu nusu ya wafungwa 223,718 waliokuwa gerezani kufikia mwishoni mwa 2018, ni vijana wa chini ya umri wa miaka 25.

Vijana wa umri wa kati ya miaka 16 na 25 ndio wamejazana katika magereza, kwa mujibu wa ripoti hiyo.

Idadi ya watoto wa chini ya miaka 16 ni ya chini japo inaonekana kuongezeka.

Kwa mfano, katika mwaka wa 2016 kulikuwa na vijana 111 wa chini ya umri wa miaka 16 waliozuiliwa magerezani, 114 mnamo 2017 na 131 mwaka jana.

Vijana wa kiume ndio wengi magerezani ikilinganishwa na wenzao wa kike.

Ukitathmini kwa makini utabaini kwamba wengi wa watu waliojazana gerezani walipatikana na hatia ya wizi na ulanguzi wa dawa za kulevya.

Inasikitisha kwamba vijana wanaofaa kuwa shuleni wakisoma ili kusaidia familia zao katika siku za usoni, wanateseka gerezani!

Kuwepo kwa idadi kubwa ya vijana wa umri wa chini magerezani ni ishara kwamba jamii imewatelekeza watoto haswa wa kiume.

Katika siku za hivi karibuni, kumekuwa na ripoti kuhusu ongezeko la vijana wa umri wa chini wanaojiunga na uhalifu.

Je, ni nini kinasababisha watoto kujiingiza katika magenge ya uhalifu?

Wengi watadai kwamba hali hiyo inasababishwa na ukosefu wa ajira nchini. Lakini ukweli ni kwamba katiba imepiga marufuku ajira za watoto wa chini ya umri wa miaka 18 kwani wanastahili kuwa shuleni.

Wazazi wametelekeza watoto wao na wameshindwa kufunza maadili mema.

Serikali haina budi kufanya utafiti ili kubaini kinachosababisha vijana kujazana katika magereza.

You can share this post!

NGILA: Tusikubali kutekwa na wajuzi ‘majambazi’ wa...

GWIJI WA WIKI: Shisia Wasilwa

adminleo