• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 8:27 PM
Tulitishwa kwa kufuta ushindi wa Rais Kenyatta, Jaji Mwilu afichua

Tulitishwa kwa kufuta ushindi wa Rais Kenyatta, Jaji Mwilu afichua

Na CHARLES WASONGA

HATIMAYE Jaji mmoja wa Mahakama ya Juu ameungama kuwa walipokea vitisho baada ya kubatilisha ushindi wa Rais Uhuru Kenyatta katika uchaguzi mkuu wa Agosti 8, 2017.

Kulingana na Naibu Jaji Mkuu (DCJ) Philomena Mwilu, vitisho hivyo havikuathiri utendakazi wao katika kesi zingine za aina hizo walizozishughulikia.

“Vitisho hivyo havikuyumbisha kwa njia yoyote maamuzi yangu kuhusu kesi zilizofuatia,” Jaji Mwilu alisema Jumanne alipohutubu katika semina ya wabunge kuhusu yaliyojiri katika uchaguzi mkuu uliopita.

“Vitisho hivyo, havikuingia rohoni mwangu. Na nashukuru Mungu kwa hilo. Nina hakika kuwa vitisho hivyo havikuathiri maamuzi mengine tuliyotoa,”akasisitiza Jaji Mwilu.

Suala hilo liliibuliwa na Mbunge wa Kapenguria Bw Samuel Moroto alimtaka DCJ kueleza ikiwa uamuzi wa kufutiliwa mbali kwa ushindi wa Rais Kenyatta ulichangia yeye na wenzake watatu, kupokea vitisho.

“Tulitishwa, hiyo ni kweli kabisa. Sharti nikubali kwa sababu sijui kuficha ukweli,” akafichua.

 

Dereva kupigwa risasi

Baada uamuzi wa kesi hiyo, iliyowasilishwa na kiongozi wa upinzani Raila Odinga, kutolewa dereva wa DCJ Mwili alipigwa risasi na watu wasiojulikana majambazi katika mtaa wa Hurlingham, Nairobi.

Kisa hicho kilitokea mnamo Jumanne Oktoba , 24 2017 siku mbili kabla ya kuandaliwa kwa marudio ya uchaguzi wa urais wa Oktoba 26. Matokeo ya uchaguzi huo pia ulipingwa na aliyekuwa Mbunge wa Kilome Harun Mwao pamoja na mwanaharakati Njonjo Mue.

 Baada ya kisa hicho, madai yaliibuliwa kuwa majambazi hao walikuwa wakilenga kumuua Jaji huyo kuhusiana na kubatilishwa kwa ushindi matokeo ya uchaguzi wa urais.

Bi Mwilu ni miongoni mwa Majaji wanne waliounga mkono kufutuliwa kwa ushindi wa Rais Kenyatta. Wengine walikuwa Jaji Mkuu David Maraga na majaji Isaac Lenaola na Smokin Wanjala.

Hata hivyo, majaji Jackton Boma Ojwang’ na Njoki Ndung’u walipinga uamuzi huo na kudumisha ushindi wa Rais Kenyatta.

Wawili hao walisema uchaguzi wa urais uliendeshwa kwa njia huru, haki na iliyozingatia katiba na sheria husika za uchaguzi, kauli ambayo pia iliungwa mkono na waangalizi wa uchaguzi kutoka mataifa ya kigeni.

You can share this post!

Mzozo wa kilabu cha Simmers: Mmiliki ataka wakurugenzi...

Hakuna pesa serikalini, Rotich aungama

adminleo