• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Ndani kwa kunaswa wakiuza vileo Kibera bila leseni

Ndani kwa kunaswa wakiuza vileo Kibera bila leseni

Na BENSON MATHEKA
WATU watatu,  walitozwa faini ya Sh50,000 kila mmoja kwa kupatikana wakiuza pombe bila leseni jijini Nairobi na wengine wawili wakatozwa faini ya Sh40,000 kila mmoja kwa kuuza pombe kabla au baada ya saa zilizowekwa kisheria.

Waliopatikana wakiuza pombe bila leseni watafungwa jela miezi sita wakishindwa kulipa faini hiyo na waliokiuka masharti ya leseni zao watafungwa jela miezi mitano.

Hakimu Mkazi wa Kibera Jane Mutuku aliwapa washtakiwa adhabu hiyo walipokiri mashtaka yaliyowakabili.

Bi Jane Mwende na Catherine Njoki walikiri kwamba walipatikana katika eneo la Ngumo mtaani Kibera wakiuza pombe kinyume na kanuni za leseni zao.

Mahakama iliambiwa kwamba walipatikana wakifungua baa kabla au baada ya muda ambao wanaruhusiwa kufanya hivyo.

Nao Mary Mutheu, Douglas Muthama na Nicholas Muriuki walikiri kwamba walikamatwa eneo la Makina Kibera wakiuza pombe bila leseni.

Upande wa mashtaka ulisema kwamba washtakiwa walikamatwa kwenye msako uliofanywa na maafisa wa polisi. Kiongozi wa mashtaka Charles Mogaka aliomba washtakiwa wachukuliwe kama wakosaji wa kwanza kwa sababu hakuwa na rekodi zao za uhalifu.

Akiwahukumu, hakimu alisema japo washtakiwa walisema walijuta kwa makosa yao, ni muhimu kufuata sheria zilizowekwa katika biashara yoyote ile.

You can share this post!

NYOTA YAKO: MACHI 08, 2018

Trump akiri Urusi iliingilia uchaguzi wa Amerika 2016

adminleo