• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 4:31 PM
USWAHILINI: Ni kweli miwa yaweza kutumiwa kudhibiti Chikungunya?

USWAHILINI: Ni kweli miwa yaweza kutumiwa kudhibiti Chikungunya?

Na LUDOVICK MBOGHOLIi

Jamii inapokabiliwa na ugonjwa unaozuka ghafla na kuathiri watu , inatafuta mbinu kuhakikisha hauenei ukasababisha maafa. Hali hii ilikumba maeneo ya Uswahilini baada ya ugonjwa ‘mpya’ wa ‘kigeni’ kuzuka na kuathiri jamii Kisiwani Mombasa.

Ugonjwa huu wa ‘Chikungunya’ ulizuka ukahangaisha jamii kiholela huku waathiriwa wakiupuuza na kupuuza ushauri wa wataalamu na maafisa wa afya. Ilibainika walioathirika waliupuuza wakiamini unatibiwa tu na dawa za kawaida.

Hata hivyo kadri siku ziliposonga , ‘Chikungunya’ ilienea kwa kasi huku waathiriwa wakihangaika wasijue tiba halisi ni ipi.

Wataalamu na maafisa wa afya walifanya utafiti wakagundua ugonjwa huo ulienezwa na aina ya mbu wasiokuwa wa kawaida. Walidai mbu hao walitoka ng’ambo wakiwa ndani ya meli wakisafiri na abiria au mabaharia wa kigeni.

Kwa mujibu wa wataalamu Uswahilini, mbu hao huzaana kwa kasi kwenye maji safi yasiyokuwa ya chumvi, ya vidimbwi au ya mabwawa na visima. Kwa utafiti wao, walidai mbu hao waliathiri idadi kubwa ya watu huko walikotoka na ni nadra kupatikana Uswahilini!

Ugonjwa huo ulipobainika , maafisa wa afya walianza mikakati ya kuudhibiti.

Ilisadikiwa mtu akiathiriwa anapooza viungo vyote mwilini ashindwe kutembea, kuongea vyema na kufanya lolote!

Unamfanya alegee na ashindwe kula vyema huku akishinda tu kitandani –Waswahili wakaupatia jina la ‘ugonjwa wa mahaba’ kwa sababu mwathiriwa hushinda kitandani asiweze kujishughulisha!

Lakini watabibu wa kienyeji nao walijibidiisha kutafuta jinsi ya kuukabili , wakagundua ili kuupunguza kasi ya kusambaa mwathiriwa anahitaji ‘kutafuna miwa’ au kunywa ‘marami’ (maji ya miwa iliyosagwa).

Watabibu hao waliarifu mwathiriwa anastahili kunywa gilasi tatu za ‘marami’ kila siku kwa siku saba mfululizo ili kupunguza kasi ya ‘Chikungunya’! Inadaiwa walioathiriwa na kufuata ushauri huo wa kienyeji walifanikiwa kuupunguza kasi ilihali waliopuuza walisalia hospitalini wakitibiwa!

Hata hivyo , inadaiwa maafisa wa afya waliarifu waathiriwa wanywe maji mengi kila siku kwani kufanya hivyo ni kuupunguza kasi yake mwilini na kuzuia maafa ya vifo.

Waliarifu tiba ya ‘Chikungunya’ ni kupata dawa za kupunguza maumivu makali mwilini na kunywa maji mengi kila saa ingawa ugonjwa huo hutesa mwili bila kusababisha vifo!

 

You can share this post!

NDIVYO SIVYO: Idadi nne za asili ya kigeni hazichukui...

Mabilionea nchini waongezeka licha ya serikali kulia haina...

adminleo