• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 4:55 PM
Mwanamume aliyepatikana na hatia ya kunajisi wasichana wawili asukumwa jela maisha

Mwanamume aliyepatikana na hatia ya kunajisi wasichana wawili asukumwa jela maisha

Na LAWRENCE ONGARO

MWANAMUME mmoja amepokezwa adhabu ya kifungo cha maisha gerezani baada ya kupatikana na hatia ya kuwanajisi wasichana wawili wadogo.

Alhamisi, Mahakama ya Thika ilimpata na makosa James Waita, 36, ya kuwanajisi watoto hao.

Mshtakiwa aliyefikishwa mbele ya hakimu mkuu A. M. Maina katika ushahidi ilielezwa aliwanajisi wasichana hao baada ya kuwahadaa na kuwapeleka katika chumba chake.

Ni kwamba mnamo Januari 14, 2016, akiwa eneo la Githurai 45, Kaunti ya Kiambu, mshtakiwa alikutana njiani na wasichana hao wawili; mmoja akiwa na umri wa miaka tisa na mwingine minane.

Baadaye aliwanunulia bhajia ya Sh20 na kuwahadaa kufika kwa chumba chake.

Baada ya kutenda kitendo hicho wasichana hao walirejea nyumbani lakini hawakusema lolote.

Hata hivyo ilidaiwa kuwa mmoja wa mama wa wasichana hao alishuku msichana wake akionyesha maumivu alipotembea.

Alipomhoji zaidi alipata kuwa alikuwa amenajisiwa vibaya sehemu zake za siri.

Mahakama iliamini jinsi wasichana hao walivyoeleza walivyonajisiwa na mshtakiwa ambaye waliweza kumtambua vyema.

Ubikira

Ripoti ya daktari iliyowasilishwa mahakamani ilionyesha wazi kuwa wawili hao walinajisiwa ambapo ubikira wao ulitatizwa baada ya kutoneshwa.

Mshtakiwa akijitetea alisema ya kwamba mashtaka hayo ni ya kusingiziwa; jambo ambalo mahakama ilipuzilia mbali ikisema ni kweli alipatikana na makosa.

Baada ya hakimu kutoa uamuzi huo, mshtakiwa alionyesha uso wa huzuni jambo ambalo lilionyesha wazi kuwa alikuwa ameshtushwa na uamuzi huo mkali.

Nao wazazi wa wasichana hao pamoja na jamaa zao waliridhika na uamuzi wa mahakama wakisema kweli haki imetendeka.

You can share this post!

AFYA: Manufaa ya kula embe

Washukiwa wawili wa uwindaji haramu wanaswa Nakuru

adminleo