• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 3:53 PM
Jubilee imekufa, Kieleweke sasa wadai

Jubilee imekufa, Kieleweke sasa wadai

Na NDUNGU GACHANE

KUNDI la wabunge wa chama cha Jubilee wanaopinga azma ya Naibu Rais William Ruto kuingia Ikulu mwaka wa 2022 sasa linadai kuwa chama hicho kimekufa licha ya wandani wa Dkt Ruto kushikilia kuwa kingali imara.

Wanachama wa kundi hilo maarufu kama Kieleweke wamemtaka Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM Raila Odinga kubuni muungano mwingine kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao.

Mbunge Maalum Maina Kamanda, mwenzake wa Gatanga Nduati Ngugi na aliyekuwa Mbunge wa Mukurwe-ini Kabando wa Kabando wanasema kwamba sasa muungano kati ya mrengo wa Jubilee unaounga mkono Rais Kenyatta na ODM ndio utaleta mwamko mpya wa kisiasa nchini Kenya.

“Ili kuleta ufufuo mpya katika ulingo wa siasa, mbegu za mivutano ya kikabila zinapasa kuangamizwa ili kutoa nafasi ya kushamiri kwa mbegu ya uwiano wa kitaifa.

“Sharti tuhakikishe kuwa tunabuni uongozi utakaoshirikisha jamii zote nchini, wala si Wakikuyu na Wakalenjin pekee kwa hali hiyo inachangia kuongeza uhasama wa kikabila,” Bw Kamanda akaambia Taifa Jumapili.

Kwa upande wake Bw Kamanda alisema: “Jubilee imekufa. Ndoa yetu na Dkt William Ruto imekufa na wale wanaoitisha mkutano wa Kundi la Wabunge wa Jubilee wanafaa kusoma dalili za nyakati na kuendelea na shughuli zao nyingine badala ya kupoteza muda wao.”

Bw Ngugi alisema kwamba Rais Kenyatta na Bw Odinga wana ushawishi mkubwa wa kisiasa nchini na wataendeleza mpango wa kubuni muungano wa kisiasa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.

“Kwa kuwa viongozi hawa wawili wanashabikiwa kwingi nchini, tumependekeza kuwa Jubilee na ODM ziungane na viongozi hao wawili wawanie uchaguzi mkuu kwa tiketi moja,” akaambia Taifa Jumapili.

You can share this post!

Echesa amtoroka Ruto, aunga Mudavadi

Wakuu wa shule waanza kikao wakilia madeni

adminleo