• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 9:12 AM
Wizara ya Fedha lawamani kutofidia polisi waliofariki wakiwa kazini

Wizara ya Fedha lawamani kutofidia polisi waliofariki wakiwa kazini

Na DAVID MWERE

WIZARA ya Fedha imelaumiwa kwa kutotoa Sh1.5 bilioni za kulipa fidia maafisa wa polisi waliofariki wakiwa kazini.

Hii ni licha ya maafisa wa polisi kuwa na bima maalum iliyosimamiwa na serikali.

Lawama hizi zinajiri baada ya kuibuka kuwa Wizara ya Usalama wa Ndani ilikuwa imewasilisha ombi la kuitaka Wizara ya Fedha kutoa fedha hizo. Mnamo 2014, Serikali Kuu iliipa kampuni ya Bima ya Pioneer kibali cha kutoa huduma za bima kwa polisi na maafisa wa magereza. Serikali ilitenga Sh3.5 bilioni kuendesha mpango huo.

Malalamishi yaliyowasilishwa na familia zilizoathiriwa katika Bunge la Kitaifa yanaonyesha kuwa familia za polisi waliofariki wakiwa kazini tangu 2017 hazijalipwa fedha zozote.

Kufikia mwezi Mei mwaka huu, vifo 460 vya maafisa wa polisi vilikuwa vimeripotiwa, lakini familia zao bado hazijapokea fidia yoyote.

Zaidi ya polisi 1,200 walikuwa wamejeruhiwa wakiwa kazini kufikia wakati huo. Vifo na majeraha yaliyoripotiwa yalihusiana na ajali za barabarani, kufyatuliwa risasi, vitendo vya ugaidi kati ya masuala mengine.

Kulingana na stakabadhi za malipo zilizo na kampuni hiyo, familia ya polisi anayefariki kutokana na ajali inapaswa kulipwa mshahara wa hadi miaka minane. Hili linamaanisha kuwa kiwango hicho ni kama Sh2 milioni. Polisi anayepata ulemavu kutokana na sababu za kikazi pia anapaswa kulipwa kiasi kama hicho.

Wanaoathiriwa pia wanapaswa kulipwa Sh150,000 kama gharama ya mazishi kwa muda wa saa 24 baada ya kupokea kibali cha mazishi.

You can share this post!

Wakuu wa shule waanza kikao wakilia madeni

Barua kwa Wakenya: Amkeni mlete mageuzi

adminleo