• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 8:12 PM
TAHARIRI: Visa vya polisi kujiua nchini vichunguzwe

TAHARIRI: Visa vya polisi kujiua nchini vichunguzwe

NA MHARIRI

Tusemezane ukweli. Ongezeko la visa vya maafisa wa polisi kujitoa uhai na kuua watu wa familia zao linatisha. Kuna hatari ya visa hivi kugeuka kuwa janga la kitaifa iwapo hatua hazitachukuliwa kurekebisha hali.

Kwa kufanya chanzo cha maafisa wa polisi kugeuza silaha za kazi yao kujiangamiza ni lazima kibainishwe na hii haitawezekana ikiwa wataalamu kutoka nje ya huduma ya polisi hawatahusishwa.

Tunasema hivi kwa sababu baadhi ya maafisa wanaofungua roho zao kabla ya kujiua huwa wanalaumu presha za kazi na kudhulumiwa na wakubwa wao kazini.

Dhuluma hizi wakati mwingine huwa ni pamoja na kupokonywa wake zao na wakubwa hao, kunyimwa ruhusa na hata kukosa kupandishwa vyeo. Wengi wa wanaotekeleza visa hivi huwa ni maafisa wa vyeo vya chini ambao huwaua wakubwa wao kabla ya kujiua.

Hii inaonyesha kuwa kuna ukweli kwamba wakubwa wanawanyanyasa wadogo wao katika kikosi cha polisi. Katika hali hii, itakuwa bora serikali itafute wataalamu kutoka nje ya kikosi kutoa huduma za ushauri nasaha.

Maafisa wanaopitia wakati mgumu kwa sababu moja au nyingine, ikiwa ni pamoja na kuteswa na wakubwa wao watakuwa na nafasi ya kufungua mioyo yao bila kuwa na hofu ya kudhulumiwa na kwa kufanya hivi hali inaweza kubadilika.

Mara nyingi, wakuu wa polisi huwa wanapuuza ripoti zinazoonyesha matatizo ya maafisa wa polisi ikiwa ni pamoja na kubaguliwa wakiwa kazini na wakubwa wao.

Itabidi Inspekta Jenerali wa polisi Hillary Mutyambai kushughulikia hali hii kwa dharura kabla maafisa wake wanaokabiliwa na matatizo ya kiakili kwa sababu ya wanayopitia kazini kugeukia umma na kuwaangamiza.

Ikizingatiwa kwamba kazi yao ni ya kudumisha usalama, inafaa maslahi ya maafisa wa polisi yazingatiwe kikamilifu, wathaminiwe na kushughulikiwa wanapokabiliwa na matatizo.

Kupuuza afisa wa polisi anayesongwa na mawazo kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi au kifamilia ni hatari kwa sababu itakuwa vigumu kwake kutekeleza majukumu yake ipasavyo.

Chembilecho wahenga, ni bora kuziba ufa kwa sababu ni ghali mno kujenga ukuta. Polisi washughulikiwe kabla ya hali hiyo kubadilika na kuwa janga kubwa.

You can share this post!

WASONGA: Ufisadi usipenyezwe katika uajiri wa maafisa wa...

JAMVI: Kuondolewa kwa noti ya Sh1,000 pigo kwa kampeni za...

adminleo