• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 8:55 PM
Mimi ni kigugumizi, Jaji Mwilu afichua kuhusu maisha yake

Mimi ni kigugumizi, Jaji Mwilu afichua kuhusu maisha yake

Na WACHIRA MWANGI na PETER MWANGANGI

NAIBU Jaji Mkuu Philomena Mwilu amezungumzia maisha yake ya kibinafsi na kukiri kuwa yeye ni kigugumizi hasa baada ya kukoselewa kuhusiana na ufasaha wake wa kuongea, na jinsi alivyoibuka kuwa miongoni mwa wanawake watajika nchini.

Jaji Mwili ambaye aliapishwa Oktoba 28, 2016 na kuchukua nafasi iliyokuwa imeshikiliwa na Jaji Kalpana Rawal, ameelezea kuwa mahali alipofikia sasa pametokana na jitihada na nidhamu hata baada ya kupitia changamoto anazosema kuwa hazikustahili.

Wakenya wengi waliofuatilia kwa karibu kesi za uchaguzi wa urais 2017 wanakumbuka akikosolewa kwa mambo kadha ambayo ni pamoja na jinsi alivyokuwa akiongea.

“Mimi ni kigugumizi, Sina ufasaha wa kuongea, Siongei vyema sana, lakini naweza kupata maelezo, na ikiwa wanaonisikiliza wana utulivivu watapata kuelewa ninakoelekea,” alisema.

“Kwa hivyo, huwa ninahakikisha kuwa nina maelezo, kwa kuwa bila maelezo, nitaeleza nini wanaonisikiliza?” alieleza wanawake waliokusanyika katika hoteli ya Sarova Whitesands Resort Beach Resort, Mombasa wakati wa kongamano la Chama cha Mahasibu Wanawake (AWAK).

Hata hivyo, ingawaje anakumbwa na hali hiyo, alisema kuwa kuna watu wengi wanaohisi kuwa ana msimamo mkali.

“Nimejifunza kutotingisika, kwa sababu usipofanya hivyo watasema hakuna mwanamke anaweza kufikia hapa bila ya kusaidiwa na mwanamume chumbani, ama sehemu nyingine ya kushangaza,” alieleza.

Aliongeza, “La, hilo halikunifanyikia mimi, na halitanifanyikia. Sitahitaji mwanamume kunidumisha katika kazi hii, nitamhitaji Mungu.”

Jaji Mwilu ambaye alijiunga kama wakili wa Mahakama Kuu 1984 anasema kuwa alishangaa kusikia baadhi ya watu wakisema kuwa hawamfahamu alipokuwa akihojiwa kwa nafasi anayoshikilia sasa.

“Kuna mtu aliuliza, ‘Mwilu ni Nani’ Mbona unauliza. Mimi ni wakili, nimekuwa jaji na kufanya hili na lile,” anaeleza.

“Kuna nini ikiwa haujawahi kunisikia? Katiba inasema nini kuhusu kutobagua kwa misingi ya hali ama sababu nyingine? Inamaanisha kuwa unahitaji tu kuhitimu. Ikiwa kuna yeyote ambaye anataka kunipinga kwa kazi ninayofanya kila siku, niko tayari kupingana na mtu huyo,” anasema.

Hata hivyo, maisha hayajakuwa shwari kwake wakati wote, kwani alimpoteza babake mapema sana akiwa mtoto, jambo ambalo alisema liliibua changamoto kadha maishani mwake.

“Sikufanya vyema sana katika Darasa la Saba, na nashukuru kuwa sikufanya vyema kwa kuwa hapo ndiyo nilizinduka na kuamua kukomesha mzaha wa alama nilizopata. Kutoka hapo, sijawahi kuangalia nyuma na nimeshindana na wale bora zaidi,” anasema.

Kuhusiana na kazi anayofanya sasa, Jaji Mwilu alisema wanawake hawana nafasi sawa na wanalazimika kung’ang’ana kuweza kufikia nyadhifa za juu.

 

You can share this post!

Amerika yataja Wakenya wawili magaidi sugu wa kimataifa

TAHARIRI: Mazungumzo ni hatua nzuri ya kukuza utaifa

adminleo