• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
Kamishna motoni kwa kuhangaisha wanahabari

Kamishna motoni kwa kuhangaisha wanahabari

Na WAIKWA MAINA

BARAZA la Habari (MCK) limepuuzilia mbali agizo la Kamishna wa Kaunti ya Nyandarua, Bw Boaz Cherutich kwa vyombo vyote vya habari kuwasilisha taarifa zao kwa Shirika la Habari la Kenya (KNA) kabla ya kuzichapisha.

MCK ilieleza wasiwasi wake pia kuhusu visa vinavyoongezeka vya kuhangaishwa kwa wanahabari na maafisa wa serikali za kaunti na hata ya kitaifa.

Wiki iliyopita, Bw Cherutich alitoa agizo hilo wakati wa kongamano kuhusu vita dhidi ya ugaidi na itikadi kali za kidini mjini Ol Kalou, akisema habari zinazofikia wananchi zinafaa kufanyiwa utathmini na kuruhusiwa na KNA.

Akizungumza alipokuwa Nyandarua kuchunguza kisa ambapo wanahabari walihangaishwa na kutishiwa na maafisa wa polisi wiki iliyopita, Meneja wa Uhuru wa Wanahabari katika MCK, Bi Dinnahh Ondari alisema agizo hilo lilikuwa na lengo la kunyamazisha wanahabari.

“Agizo hilo ni la kunyanyasa vyombo vya habari na tunalipinga. Tuna uhuru wa vyombo vya habari katika nchi hii na umelindwa kikatiba,” akasema Bi Ondari.

Kwenye kisa kilichokuwa kikichunguzwa, maafisa watatu wa polisi na mmoja wa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) walihangaisha na kutishia kuwapiga risasi wanahabari waliokuwa wakikusanya habari kuhusu gari lililohusishwa na uhalifu.

Gari hilo lilichomwa katika kituo cha polisi baada ya kunaswa na wananchi. Lilipatikana Ol Kalou likiwa na watu wanne walioshukiwa kuhusika kwa uhalifu mjini Ol Kalou na Nakuru.

Bi Ondari alisema inatia wasiwasi jinsi polisi wanavyojitahidi kuzuia wanahabari kutekeleza majukumu yao.

You can share this post!

Rekodi muhimu kuhusu Sharon na Melon zakosekana hospitalini

Rais akejeliwa kwa kuzomea viongozi

adminleo