• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Viongozi wataka Uhuru atatue shida za Jubilee

Viongozi wataka Uhuru atatue shida za Jubilee

Na ERIC MATARA

KUNDI la viongozi kutoka Rift Valley limehimiza chama cha Jubilee kuandaa mkutano wa wanachama wake ili kuzima tofauti kati ya kambi za Rais Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto.

Viongozi hao walisema ni muhimu kwa Rais na naibu kuelewana na watangaze kusitisha siasa za 2022, ambazo walisema zinaathiri ajenda za serikali.

Wakiongozwa na Gavana wa Nakuru, Lee Kinyanjui, kundi la wabunge, wazee wa baraza la wazee wa Bonde la Ufa na madiwani, viongozi hao walisema wanataka mkutano wa haraka uandaliwe ili kutatua matatizo yanayokumba Jubilee.

Akizungumza katika mazishi ya mbunge wa zamani wa eneobunge la Rongai, Willy Komen, Gavana Kinyanjui alisema siasa kuhusu urithi hapo 2022 ambazo zinaendelea kwa sasa, hazina umuhimu kwani zinanyima taifa maendeleo.

“Makundi ya ‘Kieleweke’ na ‘Tangatanga’ yanagawanya taifa na hii ni hatari kwa Jubilee. Tunafaa tuandae mkutano na tujadili masuala haya,” Bw Kinyanjui akasema.

“Watakaochaguliwa katika Uchaguzi Mkuu ujao itakuwa ni kwa misingi ya kutimiza ahadi ambazo tulitoa wakati wa kampeni. Kwa sasa tunahitaji kufanya kazi ya kutimiza ahadi hizi,” akasema gavana huyo.

Wabunge waliozungumza na Taifa Leo walisema joto lililoko ndani ya Jubilee litatulizwa tu kwa kuandaliwa kwa mkutano wa viongiozi.

“Namrai Rais Kenyatta aitishe mkutano ili kumaliza hatari ya kusambaratisha chama,” mbunge wa Kuresoi Joseph Tonui akasema.

Mwenyekiti wa baraza la wazee eneo la Rift Valley, Gilbert Kabage naye alisema siasa za 2022 zinapandisha joto na hofu eneo hilo, akisema siasa za majibizano zinaathiri hali ya maisha.

You can share this post!

Wanawake waonywa dhidi ya kupaka mafuta sehemu za siri

ODM yafifia Jubilee ikivuna ngome zake

adminleo