• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 6:55 AM
Madaktari Makueni waweka historia

Madaktari Makueni waweka historia

Na PIUS MAUNDU

MADAKTARI wa upasuaji katika hospitali ya Makindu, Kaunti ya Makueni wamefanikiwa kubadilisha goti la mgonjwa lililokuwa likimsumbua kutokana na ugonjwa wa viungo.

Bi Rael Mbula, ambaye amekuwa akipata matatizo ya goti kwa miaka bila mafanikio, alikuwa amepoteza uwezo wa kutembea.

Hata hivyo, wiki iliyopita familia yake ilifika hospitalini humo, kutafuta matibabu ya kubadilishwa goti.

Katika oparesheni ya upasuaji iliyochukua saa mbili, madaktari watatu na wauguzi walimhudumia Bi Mbula, 69, hadi wakafanikiwa kumbadilisha goti lililokuwa likimsumbua.

“Ugonjwa wa viungo kuuma ulikuwa umemwathiri mgonjwa huyo sana, kiwango cha kuwa na matatizo ya kutembea. Tulimpasua na kuondoa goti kisha kumweka jingine la chuma. Kwa sasa anaendelea kupata nafuu na kufanya mazoezi ya kutembea,” Dkt James Muoki ambaye aliongoza oparesheni hiyo alisema jana.

Mama huyo aliwashukuru madaktari na watu wa familia yake kwa oparesheni hiyo, japo akisema bado anahisi uchungu kidogo katika mguu huo, hali ambayo madaktari walisema ni hatua ya kupona.

Alisema furaha yake kubwa itakuwa atakaporuhusiwa kwenda nyumbani na atembee vyema tena.

“Alikuwa akihisi uchungu mwingi katika magoti, hali ambayo ilimfanya kushindwa kutembea. Kwa miaka miwili iliyopita, hajaweza kufanya kazi kutokana na hali hiyo. Tuna furaha kuwa hii itakuwa historia atakaporejelea maisha yake ya kawaida,” akasema Julius Kivala, mwanawe Bi Mbula.

Bw Kivala alisema familia iligharamia vifaa vya chuma ambavyo aliwekwa kama goti pekee, nayo bima ya afya ya kaunti ikashughulikia mahitaji mengine.

Oparesheni hiyo ilikuwa ya kwanza ya aina yake katika kaunti hiyo, kulingana Afisa Mkuu katika idara ya Afya, Dkt Patrick Musyoki.

Dkt Musyoki alisema kuwa gharama kubwa ya oparesheni hiyo na jinsi inahitaji utaalamu ndiyo sababu hospitali nyingi za umma zinashindwa kuitekeleza.

You can share this post!

Wageni kusimamia eneo jipya la mizigo bandari ya Mombasa

Tumetoka mbali pamoja, Ruto amkumbusha Uhuru

adminleo