• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 5:29 PM
DOMO KAYA: Muacheni Bahati na ya kwake, hayawahusu ndewe wala sikio

DOMO KAYA: Muacheni Bahati na ya kwake, hayawahusu ndewe wala sikio

Na THOMAS MATIKO

ACHA niwaambieni kitu leo. Simpendi Bahati hilo nalo siwezi kukuficha. Ila sina kinyongo wala chuki naye.

Simpendi kwa nini? Kwa sababu dogo kalewa ustaa. Ana dharau na majivuno sifa ambazo sikutegemea kabisa angelikuwa nazo. Ila naelewa zilipomkutia, mara tu baada ya kuwa staa na kuanza kushika pesa.

Zamani wakati akiwa hana kitu, akiwa ni yatima, akiwa anaishi kwenye makao ya Childrens Home, naambiwa hakuwa hivi, alikuwa ni mnyenyekevu na mstaarabu.

Nilitokeaje kutompenda lakini? Pengine kwako wewe itakuwa ni kwa sababu ndogo tu ila kwangu hali ni tofauti.

Mara kadhaa nimejaribu kumhoji, hasa kwa simu lakini jamaa mara zote aniyeyusha, au atanikatia simu au ataahidi kupiga lakini haijawahi tokea.

Mpaka wa leo mahojiano hayo hatujawahi kuyafanikisha na niliishia kukataa tamaa, sio lazima nimwandike. Dogo ana dharau sana mwanzo kama hamna mazoea.

Nakumbuka akininyima nukuu ya stori fulani niliyokuwa nikimbizana nayo na keshoye akawapa masela wake tofauti wakachapisha. Ila haina neno acha tuishi hivyo.

Licha ya masaibu yangu na huyu dogo, sijawahi kumtakia mabaya katika maisha yake. Juzi kumeibuka tetesi kwamba huenda yule mtoto Heaven aliyempata majuzi na mkewe aliyemzidi umri kinoma Diana Marua, sio wake.

Tetesi zimedai kuwa Bahati alishuku yule mtoto atakuwa ni wa mchepuko na hivyo kuamua kumfanyia vipimo vya DNA chini ya maji na baada ya kupata majibu, nyumbani kwao kukawa hakukaliki.

Bahati baadaye alijitokeza na kucharukia kinoma mabloga waliochapisha hiyo stori. Aliwaomba wamwache yeye na mke wake na mwanawe. Kikweli japo simpendi huyo dogo, katika hili la familia nimejikuta nikisimama naye.

Hata kama ni lazima ‘headlines’ ziuze sio kwa dizaini hii jamani. Nazungumza kama mwandishi na pia mwanafamilia. Unapozuga kwa stori kama hizi ili uuze ‘headlines’ wakati huna ushahidi wa unachokiandika maana yake nini?

Tujifunzeni kuheshimu familia za mastaa hawa jinsi nasi tunavyopenda zetu ziheshimiwe. Hata kama kweli yule mtoto sio wa kwake, nafahamu ni stori tamu lakini kama huna ushahidi mbona uchapishe uvumi kwa malengo ya kumuumiza mtu?

Sisemi kwamba sio kweli lakini mpaka sasa hamna ushahidi wa uhakika au udokezi unaoashiria hivyo jamani.

Diana sio kwamba naye mzuri kwa sababu nafsi yangu inanifanya kusadiki kuwa ni muhuni. Ndiye aliyemtongoza Bahati, wajua.

Wakaja wakaanza kuitana ‘prayer partner’ Lakini kikubwa zaidi Diana toka mahusiano yake ya zamani ameonekana kuwapenda watu maarufu, watu ambao sura zao hazikosekani kwenye TV.

Kabla ya Bahati, alikuwa akitoka na mtangazaji wa michezo wa runingani ndio akaja kuangukia huyu dogo na sasa unacheki anavyompelekesha mbio.

Lakini pamoja na yote, naamini naye anahitaji amani yake amlee huyo mtoto mchanga ambaye ndio mwanzo ana wiki tatu. tujifunzeni kuwa na utu hata kwa maadui wetu jamani.

Uandishi mwingine wa kizushi kama huo unachomea picha waandishi wengine wanaojielewa. Kama mimi hivi. Ama ni namna gani my frens’!

You can share this post!

Mashemeji wamtaka alipe mahari kwa kurithi mke baada ya...

SHAIRI: Siasa nimekuacha, kwaheri tutaonana

adminleo