Makala

DINI: Anayekuonea wivu anajitukana kuwa hajiamini, hajui ana vipaji

July 13th, 2019 Kusoma ni dakika: 2

Na FAUSTIN KAMUGISHA

WIVU ni mtihani.

Mwenye wivu haonekani mzuri anapokufanya uonekane mbaya.

“Baadhi ya watu watakukataa, kwa sababu tu unameremeta sana kuwazidi. Hiyo ni sawa endelea kumeremeta!” alisema Nandy Hale.

Wivu unaona tabasamu lako, hauoni machozi yako. Wivu unaona kicheko chako hauoni huzuni yako.

Wivu unaona pesa zako hauoni matumizi yako.

Wivu unaona baraka zako, hauoni mateso yako. Wivu unaona kampuni yako hauoni changamoto zako. Wivu unaona kisomo chako hauoni, jasho lako.

Wivu unaona bahari hauoni miamba.

Wivu unaona mabonde hauoni milima.

Kwa kifupi anayekuonea wivu anajitukana kuwa macho yake ya akili hayaoni.

Wivu ni chanzo cha vurugu, fujo na maovu mengi katika jamii kama Biblia isemavyo. “Maana popote palipo na wivu na ubinafsi, hapo pana fujo na kila aina ya uovu” (Yakobo 3: 16).

Unapowaonea wengine wivu unatangaza udhaifu wako.

Kuonea watu wengine wivu ni kujitukana kwamba wewe hujiamini, hujui vipaji vyako.

“Katika wivu kuna kujipenda kuliko upendo kwa wengine,” François de La Rochefoucauld.

Kuwaonea wengine wivu ni kutangaza kuwa huna upendo kwa jirani.

“Ni afadhali kuonewa wivu kuliko kuhurumiwa,” alisema Herodutus. Mafanikio yanazaa maadui wenye wivu. “Chuma kinatafunwa na kutu, na wenye wivu hivyo hivyo wanatafunwa na wivu,” alisema Antisthenes.

Upande mzuri wa kuonewa wivu ni kukumbushwa vipaji ulivyo navyo, nguvu ulizonazo na uwezo ulio nao. Wanaokuonea wivu wamehesabu baraka zako, vipaji vyako, mali zako na matunda yako.

“Wivu ni ufundi wa kuhesabu baraka za mwingine badala baraka zako,” alisema Harold Coffin.

Wanaokuonea wivu wanatangaza ukubwa wako.

“Anayemwonea mwingine wivu, anakiri ukubwa wake,” alisema Samuel Johnson.

Nyumba kuwa na kitu kizuri

Wivu hauingii katika nyumba zilizo tupu (Methali ya Kidanishi).

Unapoonewa wivu ina maana nyumba yako ina kitu kizuri.

Wivu ni kuumia kwa sababu ya mafanikio ya wengine.

“Wivu ni heshima ambayo akili ya kawaida hutoa kwa akili isiyo ya kawaida,” alisema Askofu Fulton Sheen wa Amerika.

Unapowaonea wengine wivu, wivu unaongea. Unaongea juu ya jambo unalolitaka, unalolipenda na unalolichukia.

Ungejifunza toka mtu unayemwonea wivu kama usingetiwa upofu na chuki. Ukiwaonea wengine wivu, wivu unadokeza ambacho hauna katika maisha yako.

“Unaweza kuwa mwezi na bado ukazionea wivu nyota,” Gary Allan. Unapoonewa wivu jua ukweli huu, watu wanachodharau katika maisha yako wanakipenda na wangetamani kuwa nacho.

Juu ya wivu na husuda papa Fransisko alikuwa na haya ya kusema: “Wivu unaua. Hauvumilii wengine kuwa na kile ambacho sina. Na kila mara husuda unateseka, kwa sababu moyo wa mwenye husuda au mwenye wivu huteseka. Ni moyo unaoteseka! Ni mateso ambayo yanatamani kifo cha wengine. Ni mara ngapi katika jumuiya zetu – na hatupaswi kutazama mbali kuona hili – watu wanauawa kupitia wivu kwa kutumia ulimi? Watu wanamwonea wivu huyu au yule na wanaanza kusengenya – na masengenyo yanaua.”

Kwa wanandoa wivu kiasi unahitajiwa. Nimesema “kiasi.” Maji yasizidi unga, na wala usiunguze. “Wivu katika mapenzi/ndoa ni kama chumvi kwenye chakula. Chumvi kidogo inaboresha utamu, lakini ikizidi sana inaharibu utamu, na katika mazingira fulani inahatarisha maisha,” alisema Maya Angelou.

Yote yakishasemwa, tunahitaji busara kuishi na watu. “Usimeremete kuliko bwana wako,” aliandika Robert Green katika kitabu chake cha 48 Laws of Power. Usimwaibishe mkubwa wako wa kazi mbele ya watu.