• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Chama sasa chataka Kaunti ziajiri madaktari waliohitimu

Chama sasa chataka Kaunti ziajiri madaktari waliohitimu

Na WINNIE ATIENO

CHAMA cha madaktari nchini kinataka serikali za kaunti kuajiri madaktari zaidi ya 2,500 waliofuzu ili kukabiliana na uhaba wa wataalamu hao kitaifa.

Kulingana na Chama cha Wahudumu wa Matibabu na Madaktari wa Meno (KMPDU), madaktari hao walifuzu na kuhitimu katika sekta hiyo ilhali hawana kazi.

Wakiongea kwenye kongamano lao la mwaka huko Mombasa, madaktari walisema idadi ya madaktari kwa wagonjwa ni mmoja kwa kila 16,000.

Katibu Mkuu wa chama hicho, Dkt Ouma Oluga aidha alitaka serikali za kaunti kuwaajiri madaktari hao ili kukabiliana na uhaba wa wataalamu hao katika hospitali za umma.

“Kama hakuna madaktari basi hakuna huduma za afya. Magavana wanadanganywa wasiajiri madaktari lakini mtajuta wenyewe,” alionya.

Chama hicho pia kilisema kitafanya mazungumzo na madiwani na bodi za ajira katika serikali za kaunti kuhakikisha madaktari hao wanaajiriwa.

Dkt Olunga alisema changamoto katika sekta hiyo ilianza Mei mwaka 2017, wakati baraza la magavana lilitoa agizo dhidi ya kuajiri madaktari moja kwa moja.

“Agizo hilo lilitolewa kwa haraka bila ya mashauriano sasa kuna majuto. Agizo hilo limetuathiri na kusababisha uhaba mkubwa wa madaktari. Lazima madaktari waajiriwe,” Dkt Oluga alisema.

Aliwataka magavana kupuuzilia mbali agizo hilo ili madaktari waanze kuajiriwa.

“Serikali za kaunti zimeshindwa kuajiri madaktari ambao wamefuzu ilhali wataalam hao wako tayari kufanya kazi sehemu yoyote nchini ili kutoa huduma kwa Wakenya ambao ni walipa kodi,” alisema Dkt Oluga.

Alitaja kaunti za Kirinyanga, Nyeri, Laikipia na Siaya ambazo zimekumbwa na uhaba mkubwa wa madaktari.

“Ukiangalia kati ya mwaka wa 2013 hadi 2015 kulikuwa na madaktari wengi kuliko waliopo hivi sasa kwasababu wale walioaga dunia, walioaacha kazi na walioenda masomo ya juu nafasi zao bado zi wazi,” Dkt Oluga aliongeza.

Wakati huo huo, chama hicho kilipongeza serikali za kaunti 17 ikiwemo Kitui kwa kuwapandisha vyeo madaktari na Mombasa kwa kuwekeza kwa muundomsingi wa kisasa hususan wadi ya kina mama kujifungua.

Vile vile chama hicho kimeonya kuwa kimeanza kuagiza madaktari waondoke kaunti za Kirinyanga na Laikipia kufuatia mgogoro kati yao na magavana.

You can share this post!

Kaunti yaelimisha maafisa kutatua kesi za mashamba

Viongozi wapinga uuzaji wa viwanda vya sukari

adminleo