• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 3:04 PM
Tuelezwe Sh636m za bima kwa afya ya wakongwe zilivyotumika – Wabunge

Tuelezwe Sh636m za bima kwa afya ya wakongwe zilivyotumika – Wabunge

Na CHARLES WASONGA

WABUNGE wameitaka Wizara ya Afya na Hazina ya Bima ya Kitaifa ya Matibabu (NHIF) kutoa maelezo kamili kuhusu namna Sh636 milioni zilitumika kufadhili matibabu ya wakongwe chini ya mpango wa Inua Jamii katika mwaka wa kifedha wa 2018/2019.

Hii ni baada ya kufichuka kwamba wengi wa wakongwe hao hawajakuwa wakipata huduma za afya katika hospitali za serikali licha ya wao kuwa na kadi za NHIF.

Waziri Msaidizi wa Afya Rashid Amana Jumanne aliwaambia wabunge wanachama wa Kamati ya Bunge kuhusu Afya kwamba kati ya Sh2.2 bilioni zilizoetengewa mpango huo wa bima ya afya katika mwaka huo wa kifedha, ni Sh636 milioni ambazo Wizara ya Afya iliwasilisha kwa NHIF.

“Katika mwaka wa kifedha wa 2018/2019 wizara haikuwasilisha fedha zote za kufadhili huduma za afya kwa wakongwe kwa NHIF kwa sababu Hazina ya Kitaifa haikutuma fedha za kutosha. Kati ya Sh2.2 bilioni ambazo wizara iliomba ni Sh636,262,500 pekee ziliwasilishwa kwa NHIF,”akasema.

Dkt Amana alikuwa ajibu swali la Mbunge wa Nakuru Mjini Magharibi David Gikaria ambaye alitaka serikali ieleze ni kwa nini serikali ilifeli kuwasilisha fedha za huduma za matibabu kwa wakongozwe kwa NHIF baada ya wao kupewa kadi za bima hiyo.

Bw Gikaria alilalamika kwa wakongwe wengi katika eneo bunge lake hunyimwa huduma afya katika hospital za serikali licha ya wao kuwa na kadi hizo.

“Hata jana (Jumatatu) jumla wazee 17 walifika afisini mwangu wakilalamika kuwa hospitali zimekataa kuwatiba licha ya wao kuwa na kadi za NHIF. Mbona serikali ilito ahadi ambayo hawawezi kutimizia wazee?” akauliza.

Naibu mwenyekiti wa kamati hiyo Swarup Mishra alipomtaka Dkt Amana kutoa maelezo kuhusu idadi kamili ya wakongwe waliofaidi na sehemu wanakotoka.

“Jibu lako halijaturidhisha kwa sababu haujatueleza ni idadi ya wazee walioonufaika na sehemu wanakotoka ili tujue ikiwa baadhi yao wanatoka eneo bunge lake Mheshimwa Gikaria au la,” akasema Dkt Mishra.

Akijibu Dkt Amana alisema hakuwa na maelezo hayo wakati huo na akaahidi kuyawasilisha kwa kamati hiyo baada ya siku 14 kwa sababu hakuandamana na maafisa wa NHIF.

“Kwa sababu zikuandamana na maafisa wa NHIF naomba kamati hii inipe muda wa siku 14 niweze kurejea hapa na maelezo kamili juhusu namna Sh636 milioni zilitumika na idadi ya wazee waliohudumiwa,” akasema.

You can share this post!

Njama ya Tangatanga kutwaa uongozi wa Jubilee

Hatimaye Oktay ajiuzulu,Gor kutangaza kaimu kocha mpya...

adminleo