• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
MAWAIDHA YA KIISLAMU: Baadhi ya sala za sunna na fadhila zake kwa Waislamu kuzizingatia

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Baadhi ya sala za sunna na fadhila zake kwa Waislamu kuzizingatia

Na HAWA ALI

KILA sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote.

Swala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Allah Subhanahu Wata’ala ametufaradhishia sala tano kila siku. Sala ambazo ni wajibu wa kila muislamu kuzisali. Pia Allah subhanahu wataala akatuwekea sala za sunna.

Sala za sunna ni muhimu sana kuzisali kwani hujaza mapengo ya sala za faradhi ikiwa zina mapungufu siku ya Qiyama. Kwa ujumla sala ni lazima mwanadamu azisali na tuzisali kwa unyenyekevu kwa kutaraji malipo kutoka kwa Allah.

Leo katika makala hii nitazungumzia baadhi tu ya sala za sunna na faida zake kwa uchache. Miongoni mwa hizo ni :

1- Rakaa 12 za sunna

2-Raka mbili kabla ya sala ya alfajiri.

3- Sala ya dhuha.

4- Sala ya witri.

1 Fadhila ya rakaa 12 za sunna

Imesimuliwa na Bibi Ummu habibah Ramla bint Abi Sufyan(Radhia Allahu anha) amesema amemsikia Mtume wa Allah(swalla Allahu alayhi wasallam) akisema ” Hakuna mja yoyote muislamu atakaeswali kwa aijli ya Allah rakaa 12 kila siku kwa kujipendekeza na si za Fardhi ila Allah atamjengea nyumba peponi” Imepokelewa na Imam Muslim.

Mwenye kudumu na kusali rakaa hizi 12 kwa ajili ya Allah na kwa ajili ya kujipendekeza kwa mola wake basi Allah subhanahu wataala atamjengea mja huyo nyumba katika pepo yake. Ni nani asiyetaka pepo ya Allah ? Tuko wapi Umma wa kiislamu kuzikimbilia kheri kama hizi. Wako wapi wenye kushindana kwa ajili ya kupata nyumba katika pepo ya Allah ? Suala litakuja je ni zipi hizo rakaa 12 ? Jibu la suala hilo linapatikana katika hadithi ifuatayo : Bibi Aisha(Radhia Allahu anha) anasema ” Amesema Mtume wa Allah rehma na amani ziwe juu yake ” Yoyote atakaedumu na rakaa 12 usiku na mchana ataingia peponi: rakaa 4 kabla ya adhuhuri na 2 baada yake. Rakaa 2 baada ya sala ya maghrib, Rakaa 2 baada ya sala ya ishaa na rakaa 2 kabla ya sala ya alfajiri”(Imepokelewa na Tirmidhy,nasai na ibn majah).

2 Raka mbili kabla ya sala ya alfajiri

Rakaa mbili kabla ya sala ya alfajiri imetajwa ndani ya rakaa 12 za kila siku ambazo mwenye kuzisali Allah humjengea mtu nyumba katika pepo. Ila nimeamua kwa uchache kuielezea sunna hii kwani wengi wa watu wamekuwa wakiipuza. Pia Mtume swalla Allahu alayhi wasallam alikuwa akiwahimiza zaidi watu kusali rakaa hizi mbili. Na imethibiti kwamba Mtume swalla Allahu alayhi wasallam alikuwa akisoma sura ndogo ndani ya rakaa mbili hizi.

Zama hizi watu wamekuwa wakiamka bado kwa dakika chache kusaliwa sala ya alfajiri ndio mtu nae hukimbilia kusali. Au wengine husali alfajiri hali ya kuwa sala tayari imeshatoka. Rakaa mbili hizi Mtume swalla Allahu alayhi wasallam anapiga mfano wa ubora wake kuliko dunia na vilivyomo ndani yake. Dunia ina mazuri mangapi? Ina vitu vya thamani vingapi ? Lakini vyote hivyo haviwezi kuzidi thamani ya rakaa mbili kabla ya sala ya alfajiri. Imesimuliwa na Bibi Aisha (radhwiya Allahu anha) amesema Mtume(swalla Allahu alayhi wasallam)” Rakaa mbili za sunna kabla ya sala ya alfajiri ni bora kuliko dunia na vilivyomo ndani yake” Imepokelewa na Imam Muslim na Tirmidhi.

Wito kwa wenye kusali sala ya alfajiri na kutojihimu na rakaa mbili hizi tusiache kukimbilia kheri kama hizi. Na wito wangu kwa wenye kulala wakati wa sala ya alfajiri unampita jua kwamba utaenda kuulizwa kwa Allah juu ya kila sala iliyokupita na pia unakosa nafasi za kheri kama hizi kwa kufuata matamanio ya nafsi yako pamoja na shetani.

3 Sala ya dhuha

Sala ya dhuha ni sala ambayo husaliwa robo saa baada ya kuchomoza kwa jua na mwisho wake ni kabla ya kuingia kwa adhuhuri. Swala huswaliwa rakaa mbili mbili hadi kufikia nane. Na imethibiti zaidi kuwa Mtume swalla Allahu alayhi Wasallam alikuwa akisali rakaa nne. Hii ni sunna ambayo wengi wa watu wameisahau labda kwa sababu ya maisha au kughurika na dunia na starehe zake. Je ni yapi malipo kwa mwenye kusali dhuha? Atakaeswali Dhuha kachukuliwa dhamana na Allah ya kusimamiwa mambo yake kwa siku ile kama anavyosema Mtume swalla Allahu alayhi wassalam katika hadithi ilopokelewa na Uqba bin Amir radhia Allahu anhu kuwa Amesema Allah kumwambia mwanadamu: Ewe mwanadamu nitosheleze mwanzo wa mchana kwa rakaa nne nami nitakutosheleza mwisho wa mchana” Imepokelewa na Imam Ahmad .

4 Sala ya witri

Imesimuliwa na Jabir radhiallahu anhu amesema: Amesema Mtume sallahu alayhu wasslam “Atakaehofu kutosimama mwisho wa usiku, basi aswali witri mwanzo wa usiku, na anayetarajia kuwa atasimama mwisho wa usiku basi na aswali witri mwisho wake, kwani witri mwisho wa usiku ni yenye kushuhudiwa na inayohudhuriwa (na malaika) na hiyo ndio bora” Imepokelewa na Imam Muslim, Tirmidhi na wengineo.

Sala ya witri ina faida kubwa sana na malipo makubwa. Yatosha fadhila yake kuwa sala ya witri inashuhudiwa na malaika. Pia ni katika wasia alousia Mtume Muhammad (swalla Allahu alayhi wasallam) kama tulivyoeleza katika hadithi iliyopita. Witri ni 1,3,5,7,11. Mtu anasali rakaa 2. Halafu anamalizia 1. Au anasali rakaa 2 halafu tena 2 halafu anamalizia moja.

Kwa ujumla sala zote zina faida kwetu waislamu. Ni wajibu wote tujihimu na kuacha uvivu katika kuzisali sala hizi. Tunamuomba Allah atujaalie miongoni mwa wale watakaosali na kukubaliwa sala zao. Na wale wenye kukumbushwa kheri na kuzikimbilia kheri hizo. Aaamin.

Allah ni mjuzi zaidi.

You can share this post!

KDF wateka mtaa Mombasa

Kimanzi aahidi kuvumisha Harambee Stars

adminleo