• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
MAWAIDHA YA KIISLAMU: Umuhimu wa Mwislamu kuwa na subra na ujira wake kutoka kwa Mola

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Umuhimu wa Mwislamu kuwa na subra na ujira wake kutoka kwa Mola

Na HAWA ALI

KILA sifa njema anastahiki Allaah (‘Azza Wa Jalla) Mola wa walimwengu na Mmiliki wa kila kitu, Rehma na Amani zimshukie Mtume wetu Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), Aali zake na Maswahaba wake na watangu wema hadi siku ya mwisho, ama ba’ad.

Umuhimu wa Subra umeelezwa katika Qur-aan na Sunnah, kwa kupatiwa mafundisho mbali mbali kupitia Manabii wa Allaah (‘Alayhimus Salaam) na pia kwa Maswahaba (Radhiya Allaahu ‘anhum). Allaah (Subhaanahu Wa Ta’ala) Anatueleza katika Qur-aan Tukufu.

“Na subiri, nakusubiri kwako kusiwe ila kwa sababu ya Allaah.” An-Nahl: 127

Kwa hiyo, tunaona kuwa tutapata ujira wa Subra kutoka kwa Allaah kwa kusubiri kwa ajili Yake pekee. Na hakika hakuna Subra yenye ujira isipokuwa inayokwenda sambamba na Ikhlaas kwa Allaah (Subhaanahu Wa Ta’ala) kwa kukubali na kuwa na Iymaan juu ya mitihani itakayokupata kwa kuamini kuwa Allaah Ndiye Aliyekupatia, Naye Ndiye wa kuiondosha. Allaah (SubhanaahuWa Ta’ala) Anatueleza.

“Hakika wenye subira watapewa ujira wao bila ya hisabu.” Az-Zumar: 10

Hawa watakaopata ujira bila ya hisabu ni wale watakaosubiri na kukithirisha ‘Ibaadah zao na kushukuru kwa mitihani itakapowakabili, sio kama baadhi yetu tukipatwa na mitihani basi tunavunjika mioyo kwa kuacha matendo mema na kuacha kukithirisha kumuabudu Allaah kwa kufuata shinikizo la Shaytwaan na kuzidi kupotea na kusahau fadhila ulizokuwa nazo kipindi chote cha awali.

Tunatakiwa kuiga Subra aliyokuwa nayo Nabii Ayyuub (‘Alayhis Salaam) ambayo daima inapaswa iwe ni ukumbusho kwetu sote. Inatakiwa tusome kisa hiki mara kwa mara kwa ajili ya kujikumbusha. Wengi wetu tunalalamika kwa kitu kidogo katika maisha. Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Alimpa mtihani Nabii Ayyuub (‘Alayhis Salaam) kwa namna ambayo kweli inatakiwa tujihusishe nayo na kuiga ili tuweze kupata ujira.

Iymaan yake na uvumilivu ni kitu ambacho kama sisi ni Waumini wa kweli tunapaswa kuiga na kutekeleza katika maisha yetu pindi tupatapo mitihani katika hali mbalimbali. Tunaona jinsi gani Allaah Anavyomsifia katika Qur-aan:

“…Bila shaka tulimkuta ni mwenye subira, mja mwema, kwa hakika alikuwa mnyenyekevu sana.” Swaad: 44

Na baada ya hapo nini kilifuata kwa Nabii Ayyuub (‘Alayhis Salaam) baada ya kuwa na Subra na kuendelea kuwa Mja mwema na mnyenyekevu? Allaah (SubhaanahuWa Ta’ala) Anatujulisha:

“Basi Tukamkubalia (wito wake) na Tukamuondolea dhara aliyokuwa nayo, na Tukampa watu wake na mfano wao pamoja nao. Ni rehma inayotoka Kwetu, na ukumbusho (mzuri) kwa wafanyao ‘Ibaadah.” Al-Anbiyaa: 83-84.

Subra ni nusu ya Iymaan, na humjenga Muislaam katika maisha mazuri na kuridhika katika hali ya mitihani atakayokumbana nayo, na hakika ukiwa na uvumilivu na kuwa na Subra basi Allaah Hukurahisishia mitihani kwa kuona ni kitu cha kawaida na kuridhika na hali hiyo huku ukitaraji malipo mema na mazuri zaidi toka Kwake.

Sisi kama Binaadamu tuna upungufu sana katika Iymaan zetu na ndio maana wengi wetu tunapopatwa na mitihani basi hushindwa kuwa na uvumilivu kwa maana mioyo yetu imejaa udhaifu wa Iymaan na kutokuwa na mapenzi ya kweli kwa Muumba wetu.

Kwa kuridhika na hali ya mitihani kwa kuamini kuwa Yeye Ndiye aliyetuumba na Ndiye katupatia mitihani hiyo, basi tuamini kuwa hakika Yeye Ndiye Atakayetuondoshea kwa kutupa malipo mema hapa duniani na kesho Akhera.

Na Mtume wetu (Swalla Allahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema,

“Kubakia katika subira kwa siku moja katika njia ya Mwenyeezi Mungu ni bora zaidi kuliko dunia hii na vyote vilivyomo ndani yake” (Al-Bukhaariy, Ahmad).

Tuangalie sisi wana Aadamu tumeumbwa na kuruzukiwa mambo mbalimbali ya malipo kutoka kwa Aliyetuumba, na kuturuzuku vitu mbali mbalimbali bila ya kutuhini, na hali Yeye Allaah (Subhaanahu Wa Ta’ala) ni mwenye Subra juu yetu pamoja na utukufu Alionao kwa kuendelea kutuneemesha kwa kutupatia rizki, kutusamehe na kutuhifadhi hali ya kuwa tunamkosea usiku na mchana.

Lakini, tazama Subhaana Allaah! Allaah Alivyo Asw-Swabuur, Ar-Rahiym, Ar-Razaaq kwetu sisi, na hali Yeye Ndiye Aliyetuumba na Hahitajii kitu chochote kutoka kwetu, ila sisi ndio twahitaji kutoka Kwake.

Tunatakiwa tufahamu kuwa Mja anapopatwa na mitihani mbalimbali kama misiba, mali, magonjwa na kadhalika, basi anatakiwa asubiri kwa maana Allaah (Subhaanahu Wa Ta’ala) Amempa mitihani hiyo kwa majaribio ya kumpima Iymaan yake je, atasubiri ili upate kuneemeka zaidi au atakufuru ili apotee zaidi na awe ni mtu wa mitihani daima na kuwa khasarani.

Kutoka kwa Abu Sa’iydil-Khudriyy (Radhiya Allaahu ‘anhu) kwamba, amesema Mtume (Swalla Allahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam:

“Atakayetaka kusubiri (kufanya Subra) basi Allaah Atampa Subra. Na hakupewa mtu jambo la kheri na pana kama Subra)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

You can share this post!

Odera ataja wachezaji watano wapya kwa mechi ya Victoria...

SHANGAZI AKUJIBU: Baada ya mume wa mtu kunitia mimba...

adminleo