• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 9:58 AM
JAMVI: Baada ya kumnasa Jumwa, Ruto sasa alenga kumkumbatia Sultan wa Pwani

JAMVI: Baada ya kumnasa Jumwa, Ruto sasa alenga kumkumbatia Sultan wa Pwani

Na WYCLIFFE MUIA

MUAFAKA wa kusitisha uhasama kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kinara wa NASA Raila Odinga unaendelea kuwaleta pamoja mahasimu wa kisiasa kwa matayarisho ya Uchaguzi Mkuu wa 2022.

Umoja wa viongozi hao wawili umempa Naibu Rais William Ruto mwanya wa kunyemelea ngome za upinzani ili kutafuta uungwaji mkono kutoka kwa wandani wa Bw Odinga.

Na sasa, Bw Ruto anadaiwa kumlenga Gavana wa Mombasa Hassan Joho anayechukukuliwa kuwa ‘Sultan’ wa siasa za Pwani.

Washirika wa naibu rais walidokeza kuwa Waziri wa Utalii Najib Balala ametumwa na Bw Ruto kuwaunganisha kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2022.

Siku chache baada ya Rais Kenyatta na Bw Odinga kukutana, Bw Ruto aliekea Pwani kwa ziara ya siku tatu ambapo alilakiwa kwa heshima na Wabunge wa chama cha ODM.

Baadhi ya wale waliomlaki Bw Ruto walidokezea Jamvi la Siasa kuwa naibu rais analenga kushirikiana na Bw Joho kuelekea siasa za 2022.

“Wakati Ruto alizuru Pwani, Joho alikuwa amesafiri nje ya nchi lakini naibu rais alitutuma tuongee na yeye ili tujipange kuhusu 2022,”mbunge mmoja wa Pwani asiyetaka kutajwa alisema.

Baadhi ya wachanganuzi wa siasa wanasema Joho amejikuza kisiasa kiasi cha kumnyima usingizi Bw Ruto kuhusu ndoto yake ya 2022.

 

Joho alivyong’aa

Mhadhiri wa chuo cha Pwani, Hassan Mwakimako anaamini kukosekana kwa Kalonzo Musyoka, Musalia Mudavadi na Moses  Wetang’ula katika bustani ya Uhuru wakati Bw Odinga alikula kiapo mnamo Januari 31, kulikuwa kilele cha Joho kung’aa kisiasa.

“Kile Joho alifanya siku hiyo ni sifa wapigakura wengi hutafuta kwa kiongozi. Joho aliwapiku vinara wenza wa NASA na huenda akawa na umuhimu mkubwa wa kisiasa kuwaliko kuelekea 2022,”alisema Prof Mwakimako.

Kwa mujibu wa  Maimuna Mwidau, mchanganuzi wa siasa za Pwani, utiifu wa Joho kwa Bw Odinga umepandisha hadhi yake ya kisiasa na kando na kuwa ‘Sultan’ wa Pwani, huenda akadhibiti kura za Nyanza.

Ili kudhihirisha mandhari ya kisiasa eneo la Pwani ni tulivu kwa Bw Ruto kufanya urafiki na wapinzani wake, mwenyekiti wa wabunge wa Pwani  Suleiman Dori alifichua kuwa Bw Odinga aliwashauri wakomeshe kampeni za kujitenga hata kabla ya kukutana na Rais Kenyatta mnamo Machi 9.

“Alikuwa ashatuambia tuunge ajenda ya serikali na hivyo ndio tunafanya. Kama chama, ni sharti tufuate kile kinara wetu anatuambia,”alisema Bw Dori.

Zaidi ya wabunge 10 wa ODM walimlaki Bw Ruto katika ziara yake ya kaunti za Mombasa, Kwale na Taita Taveta  huku wengine wakiahidi kumuunga mkono ifikiapo 2022.

 

Kuzamisha ndoto ya Joho

Mbunge wa Mvita Abdulswamad Nassir aliliambia gazeti moja la humu nchini kuwa, kuna juhudi zinaendelea kumshawishi Bw Ruto apangue ndoto yake ya kuwa rais 2022 na badala yake amuunge mkono Joho.

Bw Nassir ambaye ni mwandani mkubwa wa gavana huyo alisema hatua hiyo itahakikisha Ruto amekumbatiwa kikamilifu na Wapwani.
“Msimamo wetu ni wazi. Tunamtaka Ruto amuunge Joho mkono ili awanie urais 2022,” akasema.

Bw Nassir alisema wabunge wa Pwani walijadiliana na Bw Ruto kuhusu mapendekezo hayo kabla ya kuambatana naye katika ziara yake Pwani.

Hata hivyo, msemaji wa naibu rais, David Mugonyi, alipuuzilia mbali kuwepo na mipango kama hiyo.

Ili kuhakikisha ushirikiano kati ya rais na Bw Odinga una maana kwa watu wa Pwani, wabunge wa ODM walisema sharti Bw Joho ashirikishwe.

“Karibu Pwani Bw Ruto, lakini ni vyema tukufahamishe kuwa eneo hili lina kiongozi wake,” alisema Asha Hussein alipomlaki naibu rais Ijumaa iliyopita, eneo la Jomvu Kuu-Rabai .

Mbunge wa Malindi Aisha Jumwa alijipata pabaya alipomuidhinisha Ruto kuwania urais 2022, lakini alijitetea kuwa huo ulikuwa uamuzi wake binafsi.

 

Asubiri 2022

Mbunge wa Kaloleni  Paul Katana alidinda kumuidhinisha Ruto  na badala yake akamshauri angoje hadi 2022. Haya yanajiri huku ikifichuka kuwa Bw Joho kwa ushirikiano na mwenzake wa Nairobi walichangia pakubwa kuja pamoja kwa Rais Kenyatta na Bw Odinga.

Mbunge wa  Makadara George Aladwa alinukuliwa akisema kuwa, magavana hao wawili walikutana siku chache kabla ya rais na kiongozi wa ODM kufanya mazungumzo.

“Nilifanya mkutano na Sonko afisini mwake Machi 8, kabla ya rais na Raila kukutana na akanifichulia kuwa vinara hao wawili wako tayari kufanya kazi pamoja,”alisema Bw Aladwa.

Sonko anaonekana kuwa mwandani wa rais huku Joho ambaye ni naibu kinara wa chama cha ODM, akionekana kuwa mtiifu kwa Bw Odinga.

Inadaiwa Joho anaendela kumshawishi mwenzake wa Kilifi Amason Kingi kupuuzilia mbali juhudi zake za kuanzisha chama cha Pwani na badala yake amuunge mkono katika chama cha ODM.

Eneo la Pwani lenye takriban wapigakura 1.7 ni ngome ya NASA na litakuwa muhimu sana katika siasa za 2022.

You can share this post!

JAMVI: ‘Jenerali’ kutua nchini bila gwaride wala...

Pasta aalika mganga atibu wanawe walevi

adminleo