• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Wamiliki vyombo vya habari waonywa dhidi ya kudunisha wanahabari kimalipo

Wamiliki vyombo vya habari waonywa dhidi ya kudunisha wanahabari kimalipo

Na JUMA NAMLOLA

BARAZA la Vyombo vya Habari nchini (MCK) limewaonya wamiliki wa vyombo hivyo wanaowakandamiza wanahabari kimalipo kuwa litalazimika kuwanyima leseni.

Afisa Mkuu Mtendaji, Bw David Omwoyo, alisema jana kwamba kuwaacha wanahabari kwa miezi kadhaa bila mshahara kunachangia kiwango kikubwa cha ufisadi katika taaluma hiyo.

“Tuna taarifa kwamba baadhi ya wamiliki wa vyombo vya habari hawajalipa wanahabari kwa karibu miezi minne. Hili ni jambo lisilokubalika. Hawa wanahabari wana familia zinazowategemea na pia wana kodi za kulipa. Hatutakubali jambo hili,” akasema.

Bw Omwoyo alikuwa akizungumza wakati wa kupokea ripoti ya Kamati Maalum iliyoundwa kukusanya takwimu kuhusu vyama na mashirika ya wanahabari na wafanyakazi katika sekta ya uanahabari nchini.

Alieleza kuwa kwa kuwacheleweshea mishahara wanahabari au kuwalipa mshahara duni, wengi huishia kutegemea vyakula vya bure kwenye mikutano ya wanahabari au kuomba pesa.

“Unatarajia vipi mwanahabari anayehongwa kwa chakula au nauli kuandika habari isiyoegemea upande wowote? Iwapo tabia hii haitakoma, huenda tukalazimika kuwanyima vyeti vya kuwaruhusu kukata upya leseni zao,” akasema Bw Omwoyo.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Bw Mutegi Njau, alisema mojawapo ya changamoto kubwa waliyokumbana nayo wakati wa kusajili makundi ya wanahabari, ni kukosekana kwa mafunzo maalum yanayoenda na wakati.

“Tuligundua kuwa wanahabari wamejiunga katika vikundi kutegemea na majukumu wanayotekeleza. Ilibainika kuwa wengi hawajapata mafunzo yanayowafaa,” akasema.

Makundi 27 ya wanahabari yalisajiliwa.

You can share this post!

Kioja wake kubadilishana waume

Mbunge adai Moi alitawazwa na matapeli

adminleo