• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
Polisi wachunguza kifo tata cha dadake mbunge wa Githunguri

Polisi wachunguza kifo tata cha dadake mbunge wa Githunguri

DADAKE Mbunge wa Githunguri Gabriel Kago, Jane Murugi, alipatikana Ijumaa akiwa amefariki nyumbani kwake katika hali ya kutatanisha.

Maiti ya Bi Murugi, ambaye amekuwa ni muuguzi mkuu anayehudumu katika Kaunti ya Machakos, ilipatikana chooni nyumbani kwake katika mtaa wa Membley, Ruiru, Kaunti ya Kiambu, majira ya asubuhi.

Alifariki akiwa na umri wa miaka 41.

Taarifa za awali zimedokeza kuwa huenda mwendazake alijinyonga.

Hata hivyo, polisi wanashuku kuna njama ya kuficha ukweli kuhusu kifo cha Bi Murugi kwa sababu alipatikana amefariki akiwa ameketi kwenye bakuli la choo.

“Skafu iliyofungwa kwa tai ilipatikana ikining’inia kwenye dirisha la choo hicho,” Afisi Mkuu wa Polisi (OCPD) wa Ruiru Mutwiri Ringera alisema.

Mumewe, Dkt Stephen Ndoro, alisema aliamka saa kumi na moja alfajiri Ijumaa na hakumpata mkewe kitandani.

Ndoro, 38, ambaye ni daktari katika kaunti ya Makueni, alisema alienda chooni ndipo akampata mkewe amefariki.

Bi Murugi, ambaye alikuwa katika likizo ya uzazi, amemwacha mtoto mwenye umri wa miezi miwili.

Maiti yake ilipelekwa katika Hifadhi ya Maiti ya Chuo Kikuu cha Kenyatta ambako ilifanyiwa upasuaji jana jioni.

Afisa Mkuu wa Idara ya Upelelezi (DCI) Kaunti ya Kiambu Bw Ringera, Mheshimwa Kago na wabunge wengine walifika katika hifadhi hiyo saa saba kutizama maiti.

Polisi walisema watamdadisi mumewe Murugi katika uchunguzi wao kuhusu chanzo cha kifo chake.

You can share this post!

Wakazi wataka mgao katika bandari Lamu

Wizara yaagiza kufungwa kwa shule 22 Kisumu

adminleo