• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 6:47 AM
Qatar Airways yazindua safari ya ziada kutoka Doha hadi Mombasa

Qatar Airways yazindua safari ya ziada kutoka Doha hadi Mombasa

Na MAGDALENE WANJA

IDADI ya watalii nchini inatarajiwa kuongezeka hii ikiwa ni baada ya shirika la Qatar Airways kuzindua safari (trip) ya ziada kutoka Doha kwenda Mombasa.

Safari hii inafikisha tano idadi ya safari za kila wiki katika jiji la Mombasa kutoka Doha na inatarajiwa kuwaleta watalii wakati wa msimu wa sherehe za Krismasi na Mwaka Mpya.

Safari hiyo inatarajiwa kuanza Desemba 20, 2019, hadi Machi 27, 2020.

Mkurugenzi mkuu wa shirika hilo Akbar Al Baker alisema kuwa kuzinduliwa kwa safari hiyo ni mojawapo ya njia zitakazosaidia katika kudumisha uhusiano kati ya Kenya na Qatar na kutasaidia katika kuongeza nafasi za kazi katika maeneo ya Pwani mwa Kenya.

“Kufikia sasa, tuna zaidi ya safari 160 katika sehemu mbalimbali duniani na tunatarajia uhusiano mwema zaidi na nchi ya Kenya,” akasema Bw Al Baker katika taarifa.

Aliongeza kuwa shirika la Qatar Airways litahudumu safari hiyo ya ziada kwa kutumia ndege aina ya Airbus A320 ambayo ina viti 12 katika sehemu ya abiria wa kiwango cha business class na viti 120 katika sehemu ya economy class.

“Shirika hili litakuwa na jumla ya safari 26 kila wiki kati ya Doha na Kenya, zikiwemo tatu za kila siku kutoka Doha hadi Nairobi,” akasema Bw Al Baker.

Pwani mwa Kenya kuna vivutio vingi vya watalii hasa Old Town, Fort Jesus, Haller Park na Mbuga ya Kitaifa ya Mombasa Marine.

You can share this post!

BONGO LA BIASHARA: Mila kali zilisukuma kina mama Turkana...

KIU YA UFANISI: Huchumia juani kwa kuzungusha bidhaa za...

adminleo