• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
SENSA: Kaunti 14 zaongoza kwa idadi kubwa ya wanaume

SENSA: Kaunti 14 zaongoza kwa idadi kubwa ya wanaume

NA MWANDISHI WETU

JUMLA ya Kaunti 14 zina idadi kubwa ya wanaume kuliko wanawake, kulingana na matokeo ya sensa yaliyotolewa jana na Shirika la Takwimu nchini (KNBS).

Ripoti hiyo inaonyesha kuwa kaunti zote za ukanda wa Kaskazini Mashariki na baadhi za Pwani zina idadi ndogo ya wanawake ikilinganishwa na wanaume.

Hii ni licha ya takwimu za KNBS kuonyesha kuwa kuna idadi kubwa ya wanawake (milioni 24.0) ikilinganishwa na wanaume (milioni 23.5) nchini Kenya. Kaunti ya Garissa, ina wanaume 76,000 zaidi ya wanawake.

Kaunti nyingine katika ukanda wa Kaskazini Mashariki mwa Kenya zilizo na idadi kubwa ya wanaume ikilinganishwa na wanawake ni Wajir ambayo ina wanaume 49,534 zaidi, Mandera, Marsabit, Isiolo, Pokot Magharibi na Samburu.

Katika eneo la Bonde la Ufa, Kaunti za Baringo na Elgeyo Marakwet zina idadi ya juu ya wanaume ikilinganishwa na wanawake.

Kaunti ya Baringo ina wanaume 336,322 ikilinganishwa na wanawake 330,428. Kaunti ya Elgeyo-Marakwet inayoongozwa na Gavana Alex Tolgos, ina wanaume 227,317 ikilinganishwa na wanawake 227,151.

Kaunti ya Laikipia ndiyo ya pekee katika eneo la Mlima Kenya iliyo na uhaba wa wanawake.

Katika ukanda wa Pwani, Mombasa ina wanaume 610,257 ikilinganishwa na wanawake 598,046.

Hiyo inamaanisha kuwa jiji la Mombasa lina wanaume 12,000 zaidi ya wanawake.

Kaunti nyingine za Pwani zilizo na idadi ndogo ya wanawake ikilinganishwa na wanaume ni Tana River na Taita Taveta.

Kaunti ya Tana River ina wanaume 158,550 ikilinganishwa na wanawake 157,391.

Kaunti ya Taita Taveta ina wanaume 173,337 huku wanawake wakiwa 167,327.

Ripoti ya KNBS pia ilifichua kuwa kuna watu 1,524 walio na maumbile ya jinsia mbili. Kati yao 245 wanaishi jijini Nairobi na 135 katika Kaunti ya Kiambu.

Ripoti iliyotolewa na jopokazi lililobuniwa na Mkuu wa Sheria mnamo 2017 kuchunguza watu walio na jinsia mbili na kutoa mapendekezo kuhusu sera, ilikadiria kuwa watu walio na maumbile hayo ni 800.

Ni jopokazi hilo lililoongozwa na Bw Mbage Ng’ang’a lililopendekeza kuhesabiwa kwa watu walio na jinsia mbili katika sensa ya Agosti mwaka huu.

You can share this post!

MAPISHI: Jinsi ya kupika omena kwa kutia nazi

Kadhaa wanusurika kifo katika ajali Thika Superhighway

adminleo