• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 6:55 PM
Taharuki UG wafuasi wa upinzani wakikamatwa

Taharuki UG wafuasi wa upinzani wakikamatwa

Na AFP

IDADI isiyojulikana ya wafuasi wa upinzani Uganda, akiwemo aliyekuwa mgombea urais Dkt Kizza Besigye, wanazuiliwa na polisi kufuatia ghasia katika jiji kuu la Kampala zilizoshuhudiwa Jumatatu asubuhi.

Balaa ilizuka baada ya maafisa wa kulinda usalama kuzuia mkutano uliopangwa wa Forum for Democratic Change (FDC) katika Uwanja wa Mandela mjini Namboole.

Maafisa wa polisi na wanajeshi waliojihami vikali walizingira uwanja huo na kuwalazimu wanachama wa FDC waliojawa na hamaki kuandamana kuelekea makao makuu ya chama chao kwenye barabara kuu yenye shughuli nyingi ya Kampala-Jinja.

Ili kutawanya umati, polisi walitumia vitoa machozi, risasi za maji na risasi za bunduki na kusababisha vita vya kukimbizana.

Dkt Kizza Besigye, aliyekuwa rais wa FDC aliendelea kupungia umati hewani akiwa juu ya gari lake kabla ya polisi kulizuia na baadaye kulivuta katika Kituo cha Polisi cha Naggalama.

Hata hivyo, baadhi ya minyororo iliyotumika kuvuta gari la Besigye ilivunjika huku umma ukimshangilia mgombea huyo aliyewania urais mara nne.

Kisha polisi walitumia risasi za maji kumlazimisha Besigye kutoka garini mwake na kumweka katika gari la polisi, lililoondoka kwa kasi kuelekea Naggalama. Kutokana na vurugu hizo, mbunge wa Manispaa ya Kira, Ibrahim Ssemujju Nganda, alikamatwa lakini akatoweka.

Kupitia taarifa, polisi walisema FDC iliwafahamisha kuhusu mkutano ulionuiwa lakini wakashauriwa kubadilisha eneo, agizo walilopuuza.

“FDC ilitufahamisha kuhusu sherehe hiyo iliyopangwa na tukawajibu tukiwashauri wabadilishe eneo la hafla lakini wakatupuuza. Besigye alikaidi maagizo ya polisi na kuegesha gari lake barabarani katikati huku akiwazuia na kuwahangaisha watumiaji wengine wa barabara,” “Gari lilivutwa na kupelekwa katika Kituo cha Polisi cha Naggalama. Kwa sasa hakuna mashtaka aliyoshutumiwa dhidi yake lakini wapelelezi bado wanakusanya ushahidi,”alisema msemaji wa polisi Kampala Metropolitan Bw Patrick Onyango. Huku uchaguzi wa 2021 ukijongea, vyama vya kisiasa vya upinzani na makundi ya wakereketwa vinapambana kuweka mikakati ya kumkabili Museveni.

Hata hivyo, polisi kila mara wamevunja mikutano yao wakitaja ukiukaji wa Sheria kuhusu Usimamizi wa Utulivu kwa Umma.

Majuzi, Besigye na wafuasi wake kadha walizindua kampeni ya uasi wa umma inayoitwa ‘Tubalemese’, akisema itasaidia upinzani kufanikisha malengo yake.

You can share this post!

SHANGAZI AKUJIBU: Nimegundua aliyeahidi kunioa tayari ana...

Raila motoni kwa ‘kuwatusi’ mabinti Wakamba

adminleo