• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:39 PM
Polisi wasifiwa kwa juhudi za kuzima uhalifu

Polisi wasifiwa kwa juhudi za kuzima uhalifu

KALUME KAZUNGU na LUCY MKANYIKA

TUME ya Huduma kwa Polisi nchini (NPSC) imepongeza juhudi zinazoendelezwa na maafisa wa vitengo mbalimbali vya usalama katika kukabiliana na wahalifu.

Mwenyekiti wa NPSC, Bw Eliud Kinuthia, alisema kupitia juhudi hizo, Lamu kwa sasa ni miongoni mwa maeneo yanayoshuhudia amani na utulivu nchini.

Akizungumza wakati wa ziara yake kwenye maeneo mbalimbali ya Lamu mwishoni mwa juma, Bw Kinuthia aliwataka wageni, watalii na wawekezaji ambao wamekuwa wakisitasita kutembea na hata kuwekeza eneo hilo kwa sababu za kiusalama kubadili fikra zao kwani Lamu iko na usalama wa kutosha.

Akitaja sherehe ya Maulid iliyoandaliwa mjini Lamu na kukamilika Ijumaa, Bw Kinuthia alisema hafla hiyo ilivutia maelfu ya wageni na watalii kutoka sehemu mbalimbali za nchi na ulimwenguni waliofika Lamu kujumuika na wenyeji katika maadhimisho ya hafla hiyo.

Aliwasifu maafisa wa usalama wakiwemo wanajeshi wa nchi kavu (KDF) na wale wa vitengo mbalimbali vya polisi ambao wamejitoa kikamilifu na hata kuhatarisha maisha yao katika kudhibiti usalama wa Lamu.

“Niko na furaha kubwa jinsi Lamu ilivyodhibitiwa kiusalama. Kuna amani ya kutosha ikilinganishwa na miaka iliyopita. Ninawashukuru maafisa wetu wa usalama wanaoendeleza operesheni ya Linda Boni kwenye msitu wa Boni kwa kujitolea mhanga katika kudhibiti usalama eneo hili.

“Ningewasihi wawekezaji na watalii ambao wamekuwa wakihofia kutembea Lamu kuondoa shaka. Lamu ni shwari. Ni amani tupu hapa,” akasema Bw Kinuthia.Mwenyekiti huyo wa tume ya kuajiri polisi aidha alisema serikali itaendelea kujitolea kikamilifu katika kudhibiti usalama kote nchini ili maendeleo yaafikiwe hata zaidi.

Operesheni ya Linda Boni ilizinduliwa Septemba, 2015 baada ya kuzidi mashambulizi na mauaji ya mara kwa mara yaliyokuwa yakitekelezwa na magaidi wa Al-Shabaab dhidi ya raia na walinda usalama kwenye maeneo mbalimbali ya Lamu.

Kwingineko, zaidi ya familia kumi zinakadiria hasara baada ya nyumba zao kuharibiwa na maporomoko ya udongo katika kijiji cha Sungululu, kaunti ndogo ya Wundanyi, Taita Taveta.

Familia hizo ziliepuka mauti Ijumaa usiku baada ya udongo kuzika nyumba zao na baadhi ya mifugo na mali zingine.Wakaazi hao wanakadiria maafa hayo, huku wakisalia bila makao kutokana na mkasa huo.

Milima ya Taita imekuwa ikishuhudia mvua nyingi tangu wiki iliyopita. Wenyeji sasa wanaishi kwa hofu wakihofia maafa zaidi, huku mvua nyingi ikiendelea kunyesha katika eneo hilo.

Bi Linet Nyambu alisema kuwa alinusurika kifo baada ya kufunikwa na udongo huo. Alisema kuwa watoto wake walimuokoa baada ya kuangukiwa na udongo usiku huo.

“Nilikuwa nasaidia kuondoa vyombo ndani ya nyumba yangu ndio udongo ukaporomoka juu yangu,” akasema nyanya huyo wa miaka 70.Mwenyeji mmoja Bw Moses Mwanake alisema kuwa mifugo na kuku walikuwa wamefunikwa na udongo.

Alisema kuwa hawana mahali mbadala pa kuhamia huku mvua ikiendelea katika eneo hilo. Familia hizo sasa zimeitaka serikali kuwasaidia ili waweze kujenga nyumba zao tena.

You can share this post!

Msiwapasue watoto wa jinsia mbili, madaktari waonywa

Waliomuua mwanahabari wa The Star kushtakiwa

adminleo