• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 9:12 AM
Tangatanga sasa wakubali kueneza injili ya BBI kote nchini

Tangatanga sasa wakubali kueneza injili ya BBI kote nchini

Na LEONARD ONYANGO

WANASIASA wa Jubilee wanaounga mkono Naibu wa Rais William Ruto wametangaza kuwa wataanza kushiriki mikutano ya kuhamasisha Wakenya kuhusu ripoti ya Jopo la Maridhiano (BBI).

Wakiongozwa na Kiongozi wa Wengi katika Seneti, Kipchumba Murkomen, zaidi ya wabunge 20 wa kundi la Tangatanga Jumanne walisema watahudhuria mkutano wa BBI utakaofanyika jijini Mombasa Jumamosi hii.

Viongozi hao walifanya kikao cha faragha kabla ya kutangaza kulegeza msimamo wao.

“Tutashiriki katika mikutano ya BBI itakayofanyika kote nchini. Wikendi hii tutakuwa jijini Mombasa na kikosi cha BBI. Tutahimiza wafuasi wetu katika maeneobunge yote 290 wajitokeze na watoe maoni yao,” akasema Bw Murkomen.

Viongozi hao walisema kuwa wanalenga kuhakikisha kwamba masuala wanayoambiwa Wakenya katika mikutano hiyo kuhusu ripoti ya BBI ni sahihi.

Hatua hii ni mabadiliko kwa kundi la Dkt Ruto, ambalo limekuwa likipinga vikali mikutano inayoendelea nchini wakisema kuwa haina haja kwani hakuna mtu anayepinga ripoti hiyo.

Kufikia sasa mikutano hiyo imefanyika katika maeneo ya Nyanza na Magharibi.

Msimamo wa awali wa kundi hilo ulikuwa kamba wanasiasa wasiruhusiwe kuandaa mikutano ya kuhamaisha Wakenya kuhusu BBI na badala yake jukumu hilo liachiwe jopokazi la watu 14 lililoandaa ripoti hiyo.

Wanasiasa wa Tangatanga pia walikuwa wakidai kuwa mikutano hiyo inatumiwa kufuja fedha za walipa ushuru.

Pia wamekuwa wakimshutumu Kiongozi wa ODM Raila Odinga kwa madai ya kutumia mikutano hiyo kujipigia debe kwa ajili ya kinyang’anyiro cha urais 2022.

“Sasa tutashiriki kikamilifu katika mikutano ya BBI na ikibidi tutaiendesha sisi” akasema Bw Murkomen.

Juhudi za wanasiasa wa Tangatanga kutaka kuandaa mkutano sambamba na ule wa BBI uliofanyika uwanjani Bukhungu, Kaunti ya Kakamega, zilizimwa walipotawanywa na polisi.

Mikutano hiyo pia imekuwa ikitumiwa kushambuliwa mrengo wa Dkt Ruto.

You can share this post!

Mvutano wa Uhuru, Ruto watatiza kikao cha kumtimua Waititu

Oloo atetea vikao vya BBI akisema ni vya uhamasisho

adminleo