• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Moi alichukia ulevi, asema mjukuu wake

Moi alichukia ulevi, asema mjukuu wake

Na FRANCIS MUREITHI

MJUKUU wa Rais mstaafu Daniel arap Moi, amefichua kuwa babu yake alichukia pombe na hakutaka walevi wajumuike naye kamwe.

“Babu yetu (Mzee Moi) hakufurahia kumwona yeyote akiwa mlevi. Hakuna mtu yeyote wa familia yetu angethubutu kuingia nyumbani kwake akiwa mlevi,” akasema mjukuu wake, Gerald, ambaye ni mwanawe marehemu Jonathan Moi.

Akiongea na Taifa Leo jana, Gerald alisema kwa sababu Mzee Moi alichukia pombe hakuna mtu wa familia hiyo alihudhuria hafla za kifamilia akiwa mlevi.

“Wale ambao hawakuwa waraibu wa pombe walipata misaada ya kifedha kutoka kwa babu yetu kila mara. Hii ndio sababu baadhi ya wanawe Mzee walikuwa karibu naye zaidi kwa sababu aliwapenda wasio waraibu wa pombe,” akaeleza Gerald.

Alifichua kuwa endapo Mzee Moi angegundua kuwa baadhi ya wanawe au wajukuwe walikuwa wakilewa alikuwa akiwakaripia papo hapo.

“Pindi babu angegundua kuwa mmoja wetu ni mlevi angemgombeza hapo hapo na kumwelezea kuhusu madhara ya pombe,” Gerald akaeleza.

Alimtaja babu yao kama mtu aliyekuwa mkarimu na mpole na aliyependa kuwasaidia watu bila ubaguzi.

“Mzee Moi alithamini elimu na wakati huu ninasomea kozi ya Uhandisi katika Chuo cha Mafunzo ya Kiufundi cha Rift Valley mjini Eldoret kwa sababu ya usadizi wa kifedha niliopata kutoka kwake,” akasema Gerald.

Alisema watamkosa Mzee Moi haswa wakati wa mkutano ya kifamilia kila Desemba ambapo wangempa zawadi.

“Baada ya kumpa zawadi hizo angetuhubiria na kunukuu vifungu vya Biblia. Neno la Mungu ndio zawadi kuu ambayo daima nitakumbuka kupewa na babu yangu. Vile vile, alitushauri kuwaheshimu wazee na wazazi,” akasema Gerald.

Alisema mkutano wa mwisho wa Mzee Moi pamoja na wajukuu ulifanyika Desemba 2018 na alikuwa akiwakumbuka wajukuu wake wote.

“Aliwatambua wajukuu wake wote kwa majina yao licha ya umri wake mkubwa,” akasema Gerald.

You can share this post!

Kifo cha Moi chaibua makovu ya mauaji ya halaiki Wagalla

Serikali yatoa ratiba ya safari ya kumuaga Moi

adminleo