• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 12:48 PM
SEKTA YA ELIMU: Magoha atoe mipango thabiti ya mageuzi katika vyuo vikuu

SEKTA YA ELIMU: Magoha atoe mipango thabiti ya mageuzi katika vyuo vikuu

Na CHARLES WASONGA

HATUA ya Waziri wa Elimu Profesa George Magoha ya kupiga marufuku mwenendo wa vyuo vikuu vya umma kubuni mabewa sehemu mbalimbali nchini sio geni.

Vilevile, sio mara ya kwanza kwa Waziri huyo, watangulizi wake, kuviamuru vyuo hivyo vifutilie mbali kozi ambazo hazisaidii kufanikisha mipango ya maendeleo yaliyotangazwa na serikali.

Itakumbukwa kwamba mnamo mwaka 2017 aliyekuwa Waziri wa Elimu Fred Matiang’i (sasa Waziri wa Usalama wa Ndani) aliviamuru vyuo hivyo vikome kuanzia mabewa mapya na kuapa kufunga yale aliyoyataja kama “feki”.

Na alipokuwa akisoma bajeti ya kitaifa Juni 2019 aliyekuwa Waziri wa Fedha Henry Rotich alitangaza kuwa serikali inapanga kuviunganisha baadhi ya vyuo vikuu kando na kufunga mabewa kadhaa.

Alitaja hatua hiyo kama sehemu ya mageuzi ambayo serikali inapania kutekeleza katika sekta ya vyuo vikuu katika mwaka huu wa kifedha wa 2019/2020.

Hii ni baada ya kubainika kwamba baadhi ya vyuo vikuu haviwezi kujisimamia kwa sababu ya kupungua kwa ufadhili kutoka kwa serikali ya kitaifa, kupungua kwa idadi ya wanafunzi, uhaba wa vifaa vya mafunzi na wahadhiri waliohitimu.

Lakini akihutubu alipofungua rasmi kongamano kuhusu elimu ya vyuo vikuu jijini Nairobi mapema wiki hii, Profesa Magoha hakufichua mikakati ambayo wizara yake imetekeleza kufanikisha mabadiliko yaliyotangazwa awali na mawaziri wenzake.

Ni muhimu kwa Waziri huyu pia kutangaza hatua ambayo wizara yake imepiga kwamba kwa mfano, kahakikisha kuwa kozi ambazo zimetajwa na Tume ya Elimu ya Vyuo Vikuu (CUE) kama zinafaa.

Vile vile, Magoha anapaswa kutoa mipango ya serikali katika kufadhili elimu ya vyuo vikuu vya umma nchini kwani vyuo hivi vinakabiliwa na changamoto kubwa ya kifedha. Kwa mfano, mapema wiki hii, Chuo Kikuu cha Kenyatta kililazimika kukopa Sh450 milioni kutoka kwa benki baada ya kushindwa kuendesha baadhi ya mipango yake.

Hii ndiyo maana mwaka 2019 manaibu chansela wa vyuo vikuu vya umma waliitaka serikali kuongeza karo inayotozwa wanafunzi wanaofadhiliwa na serikali.

Baraza la Manaibu Chansela lilipendekeza wanafunzi hao wawe wakilipa karo ya mafunzo ya Sh48,000 kila mwaka badala ya Sh16,000 wanazolipa sasa, pendekezo ambalo lilipingwa vikali na wanafunzi.

Hii ni kwa sababu tangu 2016 idadi ya wanafunzi wanaojifadhili wenyewe (self-sponsored) imepungua kwa kiwango kikubwa baada ya idadi ya wanafunzi wanaopata alama ya C+ kwenda juu kupungua. Awali, vyuo vikuu vya umma vilikuwa vikivuna hela nyingi kutokana kwa tapo hili la wanafunzi.

Mwishoni mwa 2019 Katibu Mkuu wa Chama cha Wahadhiri wa Vyuo Vikuu (UASU) Constantine Wasonga aliiambia Kamati ya Bunge kuhusu Elimu kwamba vyuo hivyo vinakabiliwa na changamoto ya kifedha kiasi cha kushindwa kuwasilisha michango ya wahadhiri kwa hazina ya Bima ya Kitaifa ya Matibabu (NHIF) na ya pensheni (NSSF).

Isitoshe, aliiambia wanachama wa kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Tinderet Julius Melly kuwa kuwa kufikia Aprili mwaka huu vyuo hivyo havikuwa vimewasilisha jumla ya Sh481.3 milioni kwa mashirika ya akiba na mikopo ya (Saccos) hali ambayo imeathiri uwezo wa wahadhiri kupata mikopo ya kujiendeleza.

Badala ya Profesa Magoha anapaswa kutoa mpango madhubuti kuhusu ufadhili wa elimu ya vyuo vikuu, badala kutangaza marufuku kiholela.

You can share this post!

Wakazi wa Mokowe kunufaika na mradi wa ujenzi wa vyoo

Huenda huu ndio mwisho wa dunia?

adminleo