• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:33 AM
Wakazi wa Thika wazidi kuomboleza kifo cha Mundia

Wakazi wa Thika wazidi kuomboleza kifo cha Mundia

Na LAWRENCE  ONGARO

WAKAZI wa mji wa Thika wanaendelea kumuomboleza meya wa zamani wa Thika, Bw Douglas Kariuki Mundia.

Kulingana na maelezo ya familia yake, marehemu, alitoa wosia wake mapema kuwa iwapo atafariki azikwe mara moja bila maiti yake kuhifadhiwa mochari.

Wanahabari walipozuru boma lake katika mtaa wa Mundia Estate Thika leo Ijumaa, wamepokea habari ya kwamba alifariki Februari 13, 2020, na kuzikwa siku iliyofuatia Februari 14, 2020, katika kijiji cha Kang’oo, Gatundu Kaskazini.

Kulingana na mwanawe Bw Isaac Munene, baba yao Mundia aliwapa wosia wake  Julai 2016 ambapo alieleza matakwa yake kuwa kifo chake kikitokea, wamzike haraka iwezekanavyo bila kuchelewa.

“Sisi kama ‘familia nne’ tuko pamoja na hakuna mvutano wowote umekuwepo, na kwa hivyo tulimzika baba yetu kwa heshima alizohitaji,” amesema Bw Munene.

Amesema licha ya kuharakisha mazishi hayo wanapanga sherehe za kuonyesha heshima kwake pamoja na wakazi wa Thika mnamo Februari 28, 2020, katika uwanja wa michezo wa Thika Stadium.

“Tunajua kuna watu wengi walimuenzi na wangetaka kutoa heshima zao za mwisho kwa baba yetu. Sisi kama familia tumepanga kufanya misa kubwa ya kumuenzi marehemu katika uwanja huo huku tukialika marafiki wake wote,” amesema Bw Munene.

Amefafanua alikuwa anaugua kila mara kuanzia mwaka wa 2014 hadi kifo chake lakini alikuwa akifuatilia matibabu na ushauri kutoka kwa daktari.

Aliyekuwa meya wa Thika Bw David Njihia, amemsifu Bw Mundia akisema yeye ndiye baba ya mkuu wa mji wa Thika.

Marehemu Mundia amekuwa uongozini kama Meya kwa miaka 20 mfululizo ambapo ukuwaji wa mji wa  Thika umetokana na uwezo wake.

“Wakati alikuwa Meya alionyesha ujuzi wake wa kuwa kiongozi wa kutambulika baada ya kuweka miundomsingi inayoshuhudiwa kwa sasa. Alifanya kazi kwa uwajibikaji na uwazi bila mapendeleo,” amesema Bw Njihia ikiwa ni sehemu ya kutoa salamu za pole.

Amewataka viongozi wa sasa hasa madiwani – MCA waliochaguliwa kuiga mfano wake meya huyo  kwa kuwatumikia wananchi bila ubaguzi wowote.

Waandishi wa habari walipozuru  boma lake mjini Thika walipata  familia  nne za marehemu wakiwa  wamekusanyika wakitayarisha  jinsi misa ya wafu itakavyoendeshwa  katika uwanja wa Thika Stadium.

Walisema kinyume na jinsi watu walivyotarajia familia hiyo litaendelea kuwa kitu kimoja na hakuna mvutano wowote wa mali utashuhudiwa .

“Mzee wetu aliacha wosia  uliokuwa na hali ya umoja kwa kutusihi kuendelea kuishi kwa umoja amani na uelewano bila mvutano wowote,” alisema Bw Munene mmoja wa mwanaye marehemu.

You can share this post!

AKILIMALI: Alitoka jijini akajiimarisha mashambani kupitia...

Wafanyakazi 28 wa kike wahitimu na kupokezwa vyeti vya...

adminleo