• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 10:50 AM
Pigo kwa Gor Tuyisenge kukosa stakabadhi za kusafiri Afrika Kusini

Pigo kwa Gor Tuyisenge kukosa stakabadhi za kusafiri Afrika Kusini

Na GEOFFREY ANENE

GOR Mahia imepata pigo kubwa kabla ya mechi yake ya marudiano dhidi ya SuperSport United kwenye Kombe la Mashirikisho baada ya Jacques Tuyisenge, ambaye ameisaidia kushinda mechi tatu zilizopita, kukosa stakabadhi za kusafiri Afrika Kusini.

Mabao ya Mshambuliaji huyu kutoka Rwanda yalisaidia mabingwa mara 16 wa Kenya, Gor, kuzamisha Vihiga United 1-0 (Machi 31), SuperSport 1-0 (Aprili 8) na Wazito 1-0 (Aprili 11).

Yuko katika orodha ya wachezaji sita tegemeo, ambao kocha Dylan Kerr atakosa huduma zao.

Tatizo la stakabadhi za usafiri pia limefungia nje mvamizi wa Ivory Coast, Ephrem Guikan kuenda mjini Pretoria. Winga matata Godfrey Walusimbi bado amegoma kuchezea Gor hadi pale atakapolipwa ada ya uhamisho.

Kiungo Ernest Wendo yuko nje kwa sababu ya kulishwa kadi za njano katika mechi mbili zilizopita, moja dhidi ya Esperance katika Klabu Bingwa na dhidi ya SuperSport katika Kombe la Mashirikisho. Mabeki Wellington Ochieng’ na Karim Nizigiyimana wanauguza majeraha.

Mshindi kati ya Gor na SuperSport ataingizwa katika mojawapo ya makundi manne ya raundi ya 16-bora. Pia atajihakikishia tuzo ya Sh27 milioni.

You can share this post!

Kirui kujizolea mamilioni kwa kusalia kileleni mwa jedwali

Kenya yalazimishwa sare tasa na Ethiopia U-17

adminleo