• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:20 AM
Marehemu Mundia akumbukwa na watu wengi Thika

Marehemu Mundia akumbukwa na watu wengi Thika

Na LAWRENCE ONGARO

WAKAZI wengi wa Thika walihudhuria misa ya kumuenzi marehemu Douglas Kariuki Mundia aliyefariki wiki mbili zilizopita.

Bw Mundia ambaye alikuwa Meya wa mji wa Thika kwa miaka 20 alifariki Februari 13, 2020, na kuzikwa keshoye ambayo ilikuwa ni Februari 14, 2020, kulingana na matakwa yake.

Hata hivyo, familia ya marehemu ilipanga misa Ijumaa, Februari 28, 2020.

Spika wa bunge la kaunti ya Kiambu ambaye alihudhuria hafla hiyo katika uwanja wa michezo wa Thika Stadium, alimsifu marehemu Mundia kama mtu aliyejitolea kuinua mji wa Thika hadi pale ulipofikia sasa.

Ili kumkumbuka marehemu kwa njia ya heshima, Bw Ndichu alipendekeza uwanja wa michezo wa Thika ubadilishwe jina uitwe Mundia Stadium, Thika.

“Ninawahimiza madiwani wa Thika, walete mswada katika bunge la kaunti ili kupendekeza jambo hilo nami bila kuchelewa nitaidhinisha,” alisema Bw Ndichu.

Kuhusu mpango wa maridhiano wa BBI, alisema mjadala huo ni wa maana sana katika nchi hii lakini akawataka viongozi wachache wanaojaribu kuingiza siasa zao duni wakome.

“Sisi kama viongozi tunaunga mkono BBI tukijua ya kwamba Rais Uhuru Kenyatta ana nia njema na nchi yetu akitarajia kuacha Wakenya wakiwa kitu kimoja. Kwa hivyo, wale wenye nia mbaya na potovu wakome kuingiza siasa,” akasema.

Misa ilihudhuriwa na aliyekuwa wakati mmoja meya wa Nairobi kwa muda mrefu Bw Nathan Kahara, pamoja na waliokuwa madiwani wapatao wanane wa hapo awali katika mji wa Thika.

Bw Karuga Wandai ambaye ni wakili mashuhuri mjini Thika – na wakati mmoja alikuwa naibu wa meya wa Thika – alimtaja marehemu Mundia kama rafiki mkubwa na waliofanya kazi kwa uelewano.

“Marehemu alileta mabadiliko mengo katika mji wa Thika ambapo miradi mingi inayoonekana kwa sasa hapa mjini ni kutokana na juhudi zake,” alisema Bw Wandai.

Bw David Njihia aliyekuwa meya wa Thika alisema wakati wao, viongozi walifanya kazi bila kujali maslahi ya pesa bali walijitolea na nguvu zao zote.

“Tungetaka kuona mfano huo kwa wakati huu ili wananchi waweze kupata huduma kwa njia inayostahili. Hata hivyo, hayo yote yatafanikiwa tu iwapo kunakuwepo na ushirikiano,” alisema Bw Njihia.

Bw Nathan Kahara ambaye alikuwa meya wa Nairobi aliwahimiza madiwani kufanya kazi kama kitu kimoja ili kufanikisha maendeleo ya kaunti ya Kiambu.

Alishauri familia ya marehemu Mundia kuwa kitu kimoja kwa kushirikiana bila ubaguzi wowote.

“Nyinyi sasa ni kitu kimoja; msikubali kuletewa fitina na watu kutoka nje kwani ni lazima mfanye jinsi marehemu alivyotaka kuona mkiishi,” alisema Bw Kahara.

You can share this post!

MUTUA: Serikali iache masihara kuhusu virusi vya Corona

Manchester United wapata timu mteremko droo ya Uropa

adminleo