• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 11:34 AM
Kufikia Ajenda 4 Kuu za Uhuru ni ndoto – PBO

Kufikia Ajenda 4 Kuu za Uhuru ni ndoto – PBO

Na DAVID MWERE

ITAKUWA vigumu Rais Uhuru Kenyatta kutimiza Ajenda zake Nne Kuu kabla ya kuondoka mamlakani 2022 ikiwa serikali itaendelea kutotimiza malengo yake ya ukusanyaji ushuru, Idara ya Bunge inayoshughulikia masuala ya bajeti (PBO) imesema.

Idara hiyo pia iliitaka serikali ya taifa kusitisha miradi ambayo haileti faida kwa taifa hili na itekeleze mageuzi katika mashirika ya serikali.

Katika ripoti yake kuhusu Taarifa ya Sera kuhusu Bajeti (BPS) ya mwaka wa kifedha wa 2020/2021 iliyowasilishwa katika Bunge la Kitaifa na Seneti, PBO inasema malengo yaliyowekwa katika bajeti ya 2019/2020 hayatawezwa kutimizwa.

Idara hiyo inaongeza kuwa mipango ambayo imetekelezwa kufikia sasa, haijachochea maendeleo katika sekta ya utengenezaji bidhaa ambayo mchango wake katika uchumi umekuwa ukididimia.

“Kutimizwa kwa ajenda kuhusu usalama wa chakula hakujashughulikiwa ipasavyo kwa sababu uzalishaji wa chakula umekuwa ukididimia, ukubwa wa mashamba unapungua, kati ya masuala mengine,” PBO inasema katika ripoti hiyo kwa anwani ‘Shut Eye Economy’.

Sekta ya chakula inahitaji angalau Sh105.4 bilioni katika bajeti ya 2020/21 lakini ni Sh51.2 katika bejeti zilizotengewa sekta hii kulingana na BPS.

Idara ya serikali ya Nyumba inahitaji ufadhili wa zaidi ya Sh1 trilioni kwa ajili ya kujenga nyumba za gharama nafuu kufikia mwaka wa 2022.

Hata hivyo, alipofika mbele ya kamati ya Bunge la Kitaifa mnamo Alhamisi wiki hii, Waziri wa Uchukuzi na Miundomsingi James Macharia alitaja ukosefu wa rasilimali za kutosha kama kikwazo kikuu kwa azma ya serikali kutimiza lengo hilo.

Waziri alisema kufikia sasa ni nyumba 228 pekee kati ya 1,370 ambazo zilipasa kuwa zimejengwa katika awamu ya kwanza ya mpango huo.

Naye Waziri wa Fedha Ukur Yatani aliiambia Kamati ya Bunge kuhusu Uchukuzi kwamba kutokana na uhaba wa fedha, serikali haitaweza kutekeleza miradi yote ambayo ilipangiwa katika mwaka wa kifedha 2019/20.

“Hali hii imechangiwa na hali kwamba Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru (KRA) haikufaulu kutimiza kiwango lengwa cha ushuru,” akasema Bw Yatani.

Na kuhusiana na Agenda ya Afya kwa Wote (UHC), Sh11.4 bilioni zimetengwa katika mwaka ujao wa kifedha wa 2020/21. Mgao huo unapasa kuongezwa hadi Sh130.5 bilioni katika mwaka wa kifedha wa 2022/23.

Ripoti ya PBO inapendekeza kuwa mabadiliko katika Hazina ya Bima ya Matibabu (NHIF) ni muhimu katika kufanikishwa kwa ajenda ya Rais Kenyatta ya Afya Kwa Wote.

“Serikali inastahili kufanikisha mageuzi katika NHIF ili asasi hii iweze kuwawezesha wananchi kupata huduma za afya kwa gharama nafuu,” inasema.

Ripoti ya PBO pia inaisuta serikali ya kitaifa kwa kutohusisha serikali 47 za kaunti katika mpango wake wa uzalishaji wa chakula.

“Rais Uhuru Kenyatta atakuwa na wakati mgumu zaidi kutimiza Ajenda Nne ikiwa serikali haitatimiza malengo ya ukusanyaji mapato,” idara hiyo ikasema.

Baada ya kuapishwa kuingia afisini kwa kipindi cha pili mnamo 2017, Rais Kenyatta alizindua Ajenda Nne Kuu za Maendeleo.

Nguzo zake kuu ni; ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, Uzalishaji chakula toshelezi, Afya kwa Wote na ustawishaji wa sekta ya utengenezaji bidhaa.

You can share this post!

Matiang’i atosha 2022, Murathe asema

Unachotakiwa kufanya ili kiwango cha damu kiongezeke mwilini

adminleo