• Nairobi
  • Last Updated March 18th, 2024 8:55 PM
Wandani wa Ruto wataka uchaguzi

Wandani wa Ruto wataka uchaguzi

PATRICK LANG’AT na ONYANGO K’ONYANGO

WAFUASI wa Naibu Rais William Ruto sasa wanataka chama cha Jubilee kuandaa uchaguzi punde baada ya virusi vya Covid -19 kumalizika.

Msajili wa Vyama vya Kisiasa, Bi Anne Nderitu wiki iliyopita alirejesha mgogoro kuhusu mabadiliko ya Kamati ya Usimamizi Nchini (NMC) kwa chama tawala, akikitaka kisuluhishe suala hilo kivyake.

Kambi ya Dkt Ruto sasa inataka kutumia fursa hiyo kuitisha jambo ambalo wamekuwa wakimezea mate kwa muda: Uchaguzi wa maafisa wa chama, mikakati inayoonekana kumlenga Katibu Mkuu Raphael Tuju na naibu mwenyekiti aliyetangaza kujiondoa, Bw David Murathe.

“Kamati Kuu ya Kitaifa (NEC) iliyopo sasa inaweza kuzinduliwa tena kutekeleza majukumu yake na kupanga chaguzi zifanyike punde baada ya janga la Covid-19 kudhibitiwa. Kwetu sisi, inahitaji tu kiongozi wa chama kuunganisha NEC na tutakuwa tayari, hatimaye kutimiza masharti yote ya Katiba,” Naibu Katibu Mkuu wa Jubilee Caleb Kositany alieleza Taifa Leo.

Wakiongozwa na Dkt Ruto, aliyetaja mabadiliko hayo kama ya udanganyifu na haramu, watu hao wapatao 350 wanaojumuisha wabunge na maseneta 146, walimwandikia Bi Nderitu barua ya malalamishi, wakiitaka afisi yake kutokubali hatua ya kubadilisha majina hayo.

Mbunge huyo wa Soy, Bw Kositany, anayeegemea mrengo wa Naibu Rais, alisema kundi hilo lililokuwa limelalamika kwa msajili wa vyama, halioni hali ambapo watahitajika kwenda kwa Baraza la Kutatua Migogoro ya Vyama vya Kisiasa.

“Sioni sababu yoyote itakayofanya mifumo ya vyama kutofanya kazi. Hatuoni haja yoyote ya kubadilisha NMC kwa sasa, tufanye uchaguzi kisha tuketi chini ili kuibadilisha tena,” alisema. Chaguzi za Chama cha Jubilee zilizopangiwa kufanyika mnamo Machi mwaka huu, ziliahirishwa hadi tarehe isiyojulikana kufuatia mkurupuko wa Covid-19.

Kwa Dkt Ruto na wenzake, kuandaliwa kwa chaguzi hizo si hatua muhimu tu katika kuimarisha ngome yao mashinani, lakini mchakato uliocheleweshwa wa kudhibiti maafisa katika chama hicho wanaonekana kumvunjia heshima Naibu Rais.

“Rais apasa kuadhibu wale ameaminia kuendesha chama lakini sasa wanajitahidi kushirikiana na upinzani na matapeli wa kisiasa kuzamisha chama. Wahuni wasio na haya ambao sasa wanapanga kutumia masaibu ya virusi kuangusha chama sawa na jinsi walivyotaka kufanya wakati wa mazishi ya Moi,”

“Ni sharti sasa turejeshe kikamilifu chama kwa wanachama wake. Ni lazima tuwafukuze waharibifu na matapeli wote waliomo ndani waliokuwa na nia ya kusambaratisha chama. “Tuju na wenzake wanapaswa kujua tunawaandama. Tutawapa hiari ya kuondoka na ikiwa hawatabanduka, tutawafurusha,” alisema Mbunge wa Belgut Nelson Koech.

You can share this post!

Utata zaidi ripoti ikiashiria Walibora aliuawa

Serikali yakataa kulegeza kanuni za kafyu mwezi wa Ramadhan

adminleo